Serikali yainyoshea kidole KNCU
Muktasari:
- Waziri wa Kilimo nchini Tanzania, Profesa Adolf Mkenda amesema kati ya vyama 43 vya ushirika vilivyofanyiwa ukaguzi na shirika la ukaguzi na usimamizi wa vyama vya ushirika nchini (Coasco), 12 vimepata hati usiyoridhisha kikiwemo chama kikuu cha ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU).
Moshi. Waziri wa Kilimo nchini Tanzania, Profesa Adolf Mkenda amesema kati ya vyama 43 vya ushirika vilivyofanyiwa ukaguzi na shirika la ukaguzi na usimamizi wa vyama vya ushirika nchini (Coasco), 12 vimepata hati usiyoridhisha kikiwemo chama kikuu cha ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU).
Profesa Mkenda ameyasema hayo leo Jumatatu Juni 28, 2021 wakati akizungumza kwenye mkutano mkuu wa 36 wa KNCU unaofanyika mjini Moshi.
Amesema katika ukaguzi uliofanywa katika chama hicho na tume iliyoundwa na Waziri Mkuu, Kasim Majaliwa pia yalibainika madudu mengi kwenye chama hicho.
"KNCU kilikuwa chama cha kwanza Afrika cha kuunganisha wakulima, chama hiki kilibeba heshima ya ushirika nchini lakini leo nimesoma hati ya ukaguzi ya Coasco, KNCU imepata hati isiyoridhisha.”
"KNCU iliyoshika mwenge wa ushirika na kumulika hata nje ya mipaka ya Tanzania leo wamepata hati isiyoridhisha na katika taarifa ya Coasco, kati ya vyama 43 walivyovifanyia ukaguzi, 12 vimepata hati isiyoridhisha na KNCU iliyoinua watu wengi kilimanjaro kikiwemo,” amesema.
Amebainisha kuwa mbali na kupata hati isiyoridhisha, kuna tume iliundwa na Majaliwa taarifa yake inaeleza kuwa kuna uuzaji wa mali za ushirika, “ushirika ni hiari na mnatakiwa kuendesha mambo yenu bila kuingiliwa lakini isingeundwa tume hii mali zile zilizouzwa zisingerudi.”
"Tunahitaji vyama hivi vifanye kazi kidemokrasia lakini kama viongozi hawatawajibika na wataingia mikataba isiyoeleweka na kuuza mali za ushirika mtaachaje kuingiliwa na Dola?”