Tari yatakiwa tafiti kuwafikia wakulima

Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania kituo cha Tari Naliendele Dk Furtunus Kapinga (kushoto) akiwaonyesha mafuta ya maganda ya korosho Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Nchini (NDC), Meja Jenerali Ibrahim Mhona (wa pili kushoto) pamoja na makamanda waliotembelea taasisi Picha na Florence Sanawa

Muktasari:

Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Nchini (NDC), Meja Jenerali Ibrahim Mhona amewataka watafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (Tari) kituo cha Naliendele kuhakikisha kuwa tafiti zote wanazofanywa zinawafikia wakulima ili kutoa majibu ya chagamoto zinazokabili sekta ya kilimo nchini.

Mtwara. Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Nchini (NDC), Meja Jenerali Ibrahim Mhona amewataka watafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (Tari) kituo cha Naliendele kuhakikisha kuwa tafiti zote wanazofanywa zinawafikia wakulima ili kutoa majibu ya chagamoto zinazokabili sekta ya kilimo nchini.

Akizungumza wakati wa kutembelea kituo hicho cha Naliendele amesema kuwa utafiti huo unafanyakazi kubwa na unaweza kuongeza tija kwa taifa kwakuwa utasaidia wakulima kupata mazao mengi yenye tija.

Amesema kuwa kituo hicho kimepewa dhamana ya kusimamia zao la korosho, ufuta na karanga lakini wameweza kufanya tafiti kwa mazo mengine ili kuwasaidia wakulima waliopo katika mikoa ya Kusini.

“Kwakweli wamekwenda mbali wanaangalia mazao mengine kama ufuta, karanga, maharage, Migomba, chikichi, viazi na muhogo hii inapendeza kwakuwa mimi ni muumini wa utafiti nafurahi kuona utafiti wenye tija ukianza”

“Niimani yangu kuwa utafiti huu utaleta faida kubwa ili wakulima walime mazao bora ili waweze kunufaika zaidi nimefurahi kuona muunganiko wa mazao hii inaleta picha nzuri kwa taifa kwakuwa sisi tunapaswa kutoa majibu ya changamoto zinanaotukabili na kuja na majibu ya changamoto zinazoikabili wilaya”

Kanal Joseph Kigeni kutoka nchini Kenya amesema kuwa Tari inapaswa kuongeza jitihada katika utekelezaji wa tatifi ili kuhakikisha kuwa wanapata mbegu za mazao ambayo yanatoa mavuno mengi.

“Yaani Tari inapaswa kuongeza jitihada za uzalishaji wa mazao mbalimbali ili kuhakikisha kuwa wakulima wanapata mavuno mengi ili inapotokea njaa katika nchi jirani kama Kenya chakula kikawepo Tanzania ili tuweze kusaidiana nimefurahi kuona mmea mmoja ukizalisha mbegu nyingi haya ni mafanikio makubwa kwa nchi” alisema Kigen

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Tari Naliendele, Dk Furtunus Kapinga amesema kuwa utafiti unaofanywa na kiuto hicho una lengo la kutatua changamoto zinazowakabili wananchi kwa upande wa kilimo.

“Sisi kama watafiti tunafanya tafiti zenye tija ili kuwezesha wakulima nchini kupata mbegu bora  za kudhibiti, magonjwa, wadudu waharibifu  na kuongeza thamani ya mazao tumepewa dhamana hiyo na jitihada za wazi zinaonekana katiak mazao mbalimbali” amesema Dk Kapinga