TCCIA wafurahishwa na mapendekezo ya bajeti
Muktasari:
- Rais wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Paul Koyi, amesema uamuzi wa Serikali kupunguza baadhi ya tozo zilizokuwa zinaathiri sekta ya kilimo na viwanda kunachochea na kuweka mazingira wezeshi na ukuaji wa viwanda vya ndani.
Dar es Salaam. Rais wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) Paul Koyi, amesema uamuzi wa Serikali kupunguza baadhi ya tozo zilizokuwa zinaathiri sekta ya kilimo na viwanda kunachochea na kuweka mazingira wezeshi na ukuaji wa viwanda vya ndani.
Taarifa ya chemba hiyo imetolewa leo Ijumaa Juni 11,2021 ikiwa ni siku moja imepita baada ya Serikali kuwasilisha bungeni mapendekezo ya bejeti kwa mwaka 2021/2022 ya Sh36.33 trilioni.
Koyi amesema kufanya hivyo kunaonyesha kuwa nchi inaweka sera ya kulinda viwanda vya ndani ambavyo vinatumia malighafi za ndani na bidhaa zitakazotengezwa zitalinufaisha taifa moja kwa moja kupitia kodi.
“Serikali imefanya vizuri kuzuia uingizwaji holela wa bidhaa kutoka nje ya nchi kwasababu kutakuwa na usawa hali itakayochochea ushindani kati ya viwanda vya ndani na vya nje,”amesema Koyi
Koyi amepongeza utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Shirika la Ndege Tanzania (ATCL),Makaa ya Mawe Mchuchuma na Chuma Liganga na bomba la mafuta ghafi.
Amesema utekelezaji wa miradi hiyo utachochea maendeleo katika sekta binafsi, ajira na kkuendeleza viwanda pamoja na biashara kupitia miradi ya kushirikiana kati ya sekta binafsi na Serikali.
Koyi amesema katika suala la kodi licha ya kupunguzwa lakini ni vema vyombo vinavyohusika na ukusanyaji kodi vikatumia njia rafiki itakayomfanya mfanyabiashara kutimiza wajibu wake wa kulipa kodi bila kushurutishwa.
“Kwa siku za nyuma kulikuwa na malalamiko vyombo hivyo vilikuwa vinatumia nguvu kwenye ukusanyaji kiasi kwamba mfanyabiashara alikuwa anaona kulipa kodi ni kama adhabu, naiomba Serikali inawezekana kupunguza kodi isiwe shida lakini watu wanaohusika wanatakiwa kutumia njia sahihi ,”amesema Koyi