Upepo wasomba jiko Shule ya Sekondari Mkwasa, wadau waomba kutoa msaada

New Content Item (1)
Upepo wasomba jiko Shule ya Sekondari Mkwasa, wadau waomba kutoa msaada

Muktasari:

Zaidi ya wanafunzi  500 wa Shule ya Sekondari Mkwasa wilayani  Hai Mkoa wa Kilimanjaro watakosa huduma ya chakula waliyoizoea kutokana na jiko la shule hiyo kusombwa na upepo mkali ulioambatana na mvua.

Hai. Zaidi ya wanafunzi  500 wa Shule ya Sekondari Mkwasa wilayani  Hai Mkoa wa Kilimanjaro watakosa huduma ya chakula waliyoizoea kutokana na jiko la shule hiyo kusombwa na upepo mkali ulioambatana na mvua.

Shule hiyo iliyopo kijiji cha Mungushi kata ya Masama Kusini ilikumbwa na kadhia hiyo Januari 10, 2021.

Akizungumza na Mwananchi Digital leo Jumatano Januari 13, 2021 mkuu wa shule hiyo, Filipo Kiula amesema mbao zilizotumika kuenzeka jiko hilo kuoza kumechangia upepo kulisomba kirahisi.

"Tuliporudi baada shule kufunguliwa tulikuta jiko hili limesombwa na upepo mkali, tunachokifanya sasa tunatafuta namna ya kujenga jiko la muda ambalo tutaezeka kwa mabati ili kutumia.”

 “Jiko hili licha ya uchakavu wake lilikuwa na uwezo wa kuhudumia wanafunzi zaidi ya 500, kwa hiyo kulingana na hali ilivyo sasa hivi tunafanya jitihada za makusudi na za haraka ili wanafunzi hawa waweze kupata huduma ya chakula," amesema Mwalimu Kiula

Ameongeza, “tunaendelea kutafuta wadau wa maendeleo waweze kutuunga mkono ili tuweze  kukimbizana na ujenzi wa jiko jingine, hapa tayari mbunge wetu ametuahidi kutoa Sh2.7 milioni ili kuangalia namna ya kutatua tatizo hili.”

Mbunge wa Hai (CCM),  Saashisha Mafuwe aliyeahidi Sh2.7 milioni amesema, “tutawaletea vifaa kwa ajili ya ujenzi wa jiko jingine..., tunajua mambo hayawezi kwenda bila wanafunzi kula na ili wanafunzi waweze kufanya vizuri ni lazima wale, ujenzi huu utaanza mara moja ili kunusuru maisha ya watoto wetu.”