VIDEO: 18 wanusurika kifo ajali wachezaji Polisi Tanzania
Muktasari:
- Wachezaji 18 wa timu ya Polisi Tanzania waliokuwa wakitoka mazoezini katika viwanja vya TPC Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro wamenusurika kifo baada ya gari walilokuwa wamepanda kuacha njia na kugonga mti eneo la Mkababuni kata ya Arusha chini.
Moshi. Wachezaji 18 wa timu ya Polisi Tanzania waliokuwa wakitoka mazoezini katika viwanja vya TPC Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro wamenusurika kifo baada ya gari walilokuwa wamepanda kuacha njia na kugonga mti eneo la Mkababuni kata ya Arusha chini.
Kamanda wa polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa amesema ajali hiyo imetokea leo Ijumaa Julai 9, 2021 na kubainisha kuwa gari hilo lilikuwa na watu 32 wakiwemo makocha, madaktari na wachezaji hao.
Amesema waliojeruhiwa zaidi ni mchezaji Gerald Mathias ambaye amevunjika miguu yote miwili pamoja na dereva wa gari hilo, Vicent Ngonyani aliyevunjika mbavu moja.
Amebainisha kuwa majeruhi wamekimbizwa katika hospitali ya rufaa ya KCMC kwa ajili ya matibabu na kwamba chanzo cha ajali hiyo kinachunguzwa.
Ofisa uhusiano msaidizi wa hospitali ya KCMC, Joel Masawe amesema waliojeruhiwa wanaendelea na matibabu na dereva yupo katika chumba cha uangalizi maalum.