VIDEO: Ndugai adai kuwatambua kina Mdee, kuwapangia kazi za kibunge
Muktasari:
Amesema wabunge hao wataendelea na shughuli zote za kibunge, labda wakijiuzulu wenyewe.
Spika wa Bunge Job Ndugai amesema bunge litaendelea kuwatambua wabunge 19 wa viti maalum wa Chadema na wataendelea na shughuli zote zinazohusu mhimili.
Ndugai ameyasema hayo leo wakati wa kuwaapisha wabunge wateule Riziki Lulida na Humprey Polepole katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya bunge.
Spika Ndugai pia ameweka wazi kuwa wabunge hao watakuwa sehemu ya kamati za Bunge anazotarajiwa kuziunda hivi karibuni na watashiriki shughuli zote za bunge.
“Wabunge wote wa bBunge la 12 tuliowaapisha tunaendelea kuwatambua kwamba ni wabunge kamili ikiwa ni pamoja na wale wa Chadema akiwamo Aida Khenani. Nashangaa wanawasonga tu hawa 19 yule mmoja vipi, wakiweza wamfukuze lakini sisi tumeshamuapisha na tunamtambua kwamba ni mbunge.
Niwahakikishie wale 19 ni wabunge kamili labda wao wenyewe kwa kutumia utaratibu wa kikatiba waamue kujiuzulu, ila hivi karibuni nitaunda kamati na watakuwa sehemu ya kamati hizo,” amesema Spika Ndugai.