VIDEO: Ushauri wa Lowassa kwa Serikali

Muktasari:

Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa ameishauri Serikali ya Tanzania kutoa motisha kwa mashirika na taasisi zinazowahudumia wananchi maeneo ya vijijini ili kuendelea kuwasaidia kukabiliana na ugumu wa maisha.

Mwanga. Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa ameishauri Serikali ya Tanzania kutoa motisha kwa mashirika na taasisi zinazowahudumia wananchi maeneo ya vijijini ili kuendelea kuwasaidia kukabiliana na ugumu wa maisha.

Lowassa ametoa kauli hiyo jana Jumamosi Novemba 30, 2019 katika hafla iliyoandaliwa na taasisi ya Yatosha kwa ajili ya kuchangisha Sh632 milioni kuwasaidia wajane, vijana, yatima na wanaoishi vijijini.

“Kufanya kazi vijijini kuna gharama kubwa, mfano mtoto wa Kimasai tusipohangaika naye kwenda shule kule wanaona ni shauri yetu na kuna matatizo mengi sana, wanahitaji msaada kupelekwa shule na hata kuanzishiwa miradi midogo ya kuwawezesha kuufukuza umasikini.”

“Sasa mashirika na taasisi kama hizi zinaanzisha miradi ya kusaidia watu vijijini, yanapaswa kupewa motisha na Serikali kwani wanalenga mahitaji ya watu wetu vijijini ambako kwa kweli kuna changamoto nyingi,” amesema Lowassa.

Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Marystella Sendoro amesema wanatoa msaada wa elimu ikiwa ni pamoja na kulipa ada, mavazi na chakula sambamba na kuanzisha na kuendeleza miradi itakayosaidia jamii kuondokana na umaskini na uchumi tegemezi.

Kipesha Lengivido mkazi wa Karambandea Wilaya ya Mwanga amesema maeneo ya vijijini bado kuna changamoto kubwa, ikiwemo ya watoto wa kike kunyimwa fursa ya kupata elimu na kuozeshwa katika umri mdogo.