Wakulima Moshi wagawiwa miche ya kahawa

Wakulima Moshi wagawiwa miche ya kahawa

Muktasari:

Bodi ya Kahawa nchini (TCB), inakusudia kutoa miche bora zaidi ya 100,000 kwa wakulima wa  halmashauri ya Moshi vijijini, lengo likiwa kuhamasisha kilimo cha zao hilo ili kufanikisha malengo ya kuongeza uzalishaji kufikia Tani 300,000 ifikapo mwaka 2025.

  

Moshi. Bodi ya Kahawa nchini (TCB), imegawa miche bora zaidi ya 100,000 kwa wakulima wa halmashauri ya Moshi vijijini, lengo likiwa kuhamasisha kilimo cha zao hilo ili kufanikisha malengo ya kuongeza uzalishaji kufikia Tani 300,000 ifikapo mwaka 2025.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa maendeleo ya kahawa TCB, Kajiru Francis, wakati wa uzinduzi wa ugawaji wa miche hiyo  ambapo amesema utoaji wa miche hiyo ni mikakati ya kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

"Leo tunazindua ugawaji wa miche ya kahawa, hapa Uru lakini tunatarajia kugawa miche zaidi ya 100,000 Moshi vijijini, nia yetu ni kufufua kilimo cha Kahawa Kilimanjaro na kuongeza uzalishaji” amesema Kajiru

Akizungumza mratibu wa zao hilo wa Halmashauri ya Moshi vijijini, Vaileth Kisanga, amesema miche itagawanywa kwa wakulima ambao tayari wameandaa mashimo.

"Leo hapa Uru miche zaidi ya 20,000 lakini itatolewa kwa wakulima ambao wameandaa mashimo na wana maji ya kumwagilia, lakini wakulima ambao hawana maji, waendelee kuandaa mashimo na mvua zitakapoanza kunyesha watapewa miche "amesema .

Meneja Mkuu wa wa Benki ya ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KCBL), Godfrey Ng'urah, amesema ugawaji wa miche itakua endelevu na kwamba benki hiyo imetenga Sh1.5 bilioni kwa ajili ya uzalishaji wa kahawa