Wanafamilia Malkia Elizabeth watua Scotland

Muktasari:

  • Ndege inayosemekana kuwabeba wanafamilia wa malkia Elizabeth, imefika nchini Scotland ambako kiongozi huyo mkuu wa kimila wa Uingereza yupo kwenye matibabu na mapumziko kwenye kasri la Balmoral.


London. Ndege inayosemekana kuwabeba wanafamilia wa malkia Elizabeth, imefika nchini Scotland ambako kiongozi huyo mkuu wa kimila wa Uingereza yupo kwenye matibabu na mapumziko kwenye kasri la Balmoral.

Ndege hiyo inaaminika miongoni mwa wanafamilia iliyowabeba ni pamoja na Mwanamfalme William, Andrew na Edward aliyeambatana na mkewe Sophie kwa ajili ya mkesha utakaoongozwa na mwanamfalme Charles pembeni ya kitanda cha malkia.

Watoto na wajukuu wa Malkia Elizabeth wamelazimika kwenda kwenye kasri la Balmoral lililopo Scotland muda mchache tangu kasri kuu la utawala la Buckingham kutoa taarifa ya afya ya malkia huyo kuwa chini ya uangalizi wa madaktari na kumuhitaji kwenda mapumzikoni Balmoral.

Hali hiyo imeendelea kuwashtua wananchi wa Taifa hilo kubwa duniani, huku wakihoji huenda kiongozi huyo akawa kwenye hali mbaya ya kiafya.

Hali hiyo pia imesababisha Malkia kuahirisha kikao alichopanga kukifanya na Baraza la Mawaziri jana Septemba 7, 2022.