Watumishi saba Geita kizimbani kwa madai ya ubadhirifu
Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita waliofikishwa mahakamani kwa ubadhirifu wa zaidi ya Sh78.8 mlioni.
Muktasari:
- Watuhumiwa wanadaiwa kukusanya zaidi ya Sh79 milioni na kutokuziwasilisha katika Akaunti ya Serikali
Geita. Watumishi saba wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Geita, wakituhumiwa kwa makosa ya ubadhirifu na kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya Sh78.8 milioni.
Watumishi hao na vyeo vyao kwenye mabano ni Tatu Kijungu (Ofisa Hesabu), Sylvanus Michael (Mhasibu), Ladislaus Kamhanda (Ofisa Mtendaji Kata ya Nyamalimbe), Melina Buguba (Ofisa Uvuvi) na Mtani Yangwe (Mkusanya Mapato).
Watuhumiwa wengine ni Allen Kimaro (Mkusanya mapato) na Mashalla Nkwande (Ofisa Mtendaji Kata ya Kakubilo) wote watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita.
Wanatuhumiwa kwa makosa saba na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS) yaliyosajiliwa kwa nambari ECO.13145/2026,ECO.13148/2026,ECO.13149/2026,ECO.13150/2026,ECO.13151/2026,ECO.13152/2026 na ECO.13153/2026.
Taarifa iliyotolewa leo Ijumaa Juni 12,2026, na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Geita, James Ruge, amesema Watumishi hao walinaswa baada ya kufanyika kwa uchunguzi katika mifumo ya ukusanyaji mapato.
"Watuhumiwa wanadaiwa kukusanya mapato kwa njia ya mfumo (Local Government Revenue Collection Information System-LGRCIS) unaotumia mashine za Point of Sale(POS).
“Hata hivyo, hawakuwasilisha makusanyo hayo kwenye Akaunti ya Serikali kinyume na utaratibu,” imeeleza taarifa hiyo.
Ruge amebainisha kuwa makosa hayo ni kinyume na kifungu cha 28 (1) cha Sheria ya kuzuia na kupambana na Rushwa namba 11 ya 2017.