Wenye VVU watakiwa kutoacha kutumia dawa
Muktasari:
Watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi nchini Tanzania wametakiwa kuzingatia matumizi ya dawa za kufubaza virusi hivyo na kuwa wazi ili kuushinda unyanyapaa.
Moshi. Watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi nchini Tanzania wametakiwa kuzingatia matumizi ya dawa za kufubaza virusi hivyo na kuwa wazi ili kuushinda unyanyapaa.
Rai hiyo imetolewa leo Jumanne Desemba mosi, 2020 na mwenyekiti wa baraza la watu wanaoishi na VVU (Nacopha) , Leticia Mourice wakati akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi duniani ambayo kitaifa inafanyikia katika viwanja vya shule ya msingi Mandela, manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro.
Amesema hali ya unyanyapaa kwa watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi (VVU) katika jamii nchini bado iko juu na ili kuweza kuishinda changamoto hiyo ni muhimu watu wakawa wazi na kutumia dawa kwa usahihi.
"Ili kuushinda unyanyapaa ni muhimu kuanza dawa kwa wakati, mara baada ya kupima na kugundulika na maambukizi ya VVU, lakini pia wazingatie matumizi sahihi ya dawa, hii itasaidia sana kuondoa unyanyapaa.”
"Pia ni muhimu kuwa wazi, kwani unapokuwa wazi katika jamii, kunakufanya uwe huru na amani ya moyo na jamii itakuona wewe kama wengine, lakini pia itasaidia kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya ukimwi,” amesema.
Amesema changamoto zilizopo, ni pamoja na kuongezeka kwa maambukizi mapya kwa vijana walio katika umri wa kubalehe na kwamba vijana wa kike wako kwenye hatari zaidi ya kupata maambukizi kutokana na kuwa kundi linalokumbwa na vishawishi vingi.
Amesema hali hiyo inachangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo wazazi kutozungumza na vijana wao kuhusu makuzi na athari wanazoweza kuzipata endapo wataingia katika vishawishi.
Katika maadhimisho hayo yaliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi mgeni rasmi ni waziri mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa.