Mbowe: Mikutano ya hadhara haikufutwa na Magufuli pekee

Muktasari:

  • Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema uamuzi wa kuzuia mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa haukuwa wa Hayati John Magufuli pekee, bali na uongozi wa chama chake- Chama Cha Mapinduzi (CCM).




Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema uamuzi wa kuzuia mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa haukuwa wa Hayati John Magufuli pekee, bali na uongozi wa chama chake- Chama cha Mapinduzi (CCM).

Mbowe ameyasema hayo leo Jumapili, Januari 22, 2023 katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya shule ya Msingi Mukendo mjini Musoma mkoani Mara, ikiwa ni siku ya pili tangu chama hicho kizindue mikutano yake jana Jumamosi, jijini Mwnaza.

“Uamuzi wa kufunga mikutano haukuwa ya Magufuli peke yake, ulikuwa wa Magufuli, kamati kuu ya chama chake na viongozi na wanachama wa CCM walio wengi, tusikae tukasema aliyefunga mikutano ni Magufuli ni CCM na dhambi hii lazima waibebe,” amesema.

Mbowe: Mikutano ya hadhara haikufutwa na Magufuli pekee, "Huu ni utawala batili...!"

Zuio la mikutano ya hadhara lilitolewa na Rais Magufuli akiwa madarakani mwaka 2016 huku akitoa fursa kwa wabunge na madiwani kufanya mikutano kwenye maeneo yao na wengine wakitakiwa kusubiri wakati wa uchaguzi.

Zuio hilo lilidumu hadi Januari 3, 2023 wakati Rais Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi wa vyama 19 vya siasa, Ikulu jijini Dar es Salaam, alipotangaza kuliondoa zuio hilo.

Katika mkutano huo wa hadhara, Mbowe amesema CCM inaiogopa Chadema, akitolea mfano baada ya uchaguzi wa mwaka 2015 chama hicho kilitathmini namna ya kushinda, baada ya kuona hakina uwezo wa kushinda kwa haki kukabuni mbinu batili.

“Yakafanyika maamuzi ambayo yalimuhitaji mtu asiye na akili sawasawa kuyatekeleza, kuamua kuwafungia wananchi uhuru wa mnaisha yao kwa miaka saba inahitaji uwendawazimu, lakini walifanya bila aibu na wafaidika wa ubatili ule ni CCM,” amesema.

Walifanya hivyo wakitambua kile alichokisema kuwa uchaguzi wa Serikali za mitaa wasingeshinda hivyo wakaona ni vema kuengua wagombea.