Azam, Simba zatinga nusu fainali Kombe la Shirikisho CRDB
Muktasari:
- Yanga ndio bingwa mtetezi wa Kombe la Shirikisho la CRDB huku pia ikiwa bingwa wa kihistoria wa mashindano hayo ikitwaa mara tano.
Dar es Salaam. Azam FC na Simba zimetinga hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB baada ya kupata ushindi katika mechi zao za leo Jumamosi, Mei 17, 2026 zilizochezwa katika viwanja tofauti nchini.
Mkoani Kigoma katika Uwanja wa Lake Tanganyika, Azam imejihajikikishia kuingia nusu fainali kwa kuichapa Mashujaa FC kwa bao 1-0.
Bao pekee la Azam FC katika mchezo huo limepachikwa na Idd Selemani ‘Nado’ katika dakika za nyongeza za kipindi cha kwanza.
Nyota wa Azam FC, Iddy Seleman wakati akishangilia baada ya kufunga bao katika mechi ya robo fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB. Picha na Azam FC
Baada ya ushindi huo, Azam FC sasa itakutana na Yanga katika mechi ya nusu fainali ya mashindano hayo.
Yanga yenyewe ilitinga katika nusu fainali baada ya jana kuichapa JKT Tanzania kwa mabao 2-0.
Kwenye Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam, Simba imepata ushindi mnono wa mabao 4-0 mbele ya TRA United katika mechi nyingine ya robo fainali ya mashindano hayo.
Wachezaji wa Simba, Clatous Chama na Nickson Kibabage wakati wakishangilia moja ya bao katika ushindi wa 4-0 iliopata Simba dhidi ya TRA United katika mechi ya nusu fainali ya Kombe la CRDB. Picha na Simba
Mabao manne ya Simba leo yamewekwa kimiani na Clatous Chama, Anicet Oura, Selemani Mwalimu na Bashiri Kibaila.
Kwenye nusu fainali, Simba itakutana na Coasta Union ambayo jana ilipata ushindi wa mikwaju ya penalti 4-3 mbele ya Singida Black Stars.