Nabi arithi mikoba ya Fadlu Raja
Muktasari:
- Nabi anatua Raja Casablanca akiwa na rekodi ya kutwaa mataji sita akiwa Yanga, yakiwemo mawili ya Ligi Kuu Bara, mawili ya Kombe la Shirikisho (FA Cup) na mawili ya Ngao ya Jamii.
Dar es Salaam. Kocha wa zamani wa Yanga, Nasreddine Nabi, ametangazwa rasmi kuwa kocha mkuu wa Raja Casablanca ya Morocco, ikiwa ni siku chache baada ya klabu hiyo kuachana na aliyekuwa kocha wake, Fadlu Davids.
Raja imethibitisha ujio wa kocha huyo raia wa Tunisia ambaye amesaini mkataba wa kuinoa timu hiyo hadi Juni 2027 huku kukiwa na kipengele cha kuongeza muda wa ushirikiano huo.
Nabi anatua Raja Casablanca akiwa na rekodi ya kutwaa mataji sita akiwa Yanga, yakiwemo mawili ya Ligi Kuu Bara, mawili ya Kombe la Shirikisho (FA Cup) na mawili ya Ngao ya Jamii.
Huku pia akiifikisha timu hiyo ya Wananchi fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika mwaka 2023
Baada ya kuondoka Yanga, Nabi alikwenda Afrika Kusini kuifundisha Kaizer Chiefs, ambako aliisaidia kutwaa Kombe la Nedbank na kumaliza kipindi kirefu bila taji.
Uamuzi wa Raja kumchukua Nabi umefuatia kuondoka kwa Fadlu Davids ambaye alishindwa kuirudisha timu hiyo katika makali yake.
Viongozi wa Raja wanaamini uzoefu wa Nabi katika soka la Afrika na uwezo wake wa kujenga timu yenye ushindani ndio utakaosaidia kurejesha makali ya klabu hiyo katika mashindano ya ndani na kimataifa.
Kwa mashabiki wa Yanga, jina la Nabi bado lina kumbukumbu kubwa kutokana na mafanikio yake huku wengi wakifuatilia kwa karibu hatua yake mpya ndani ya moja ya klabu kubwa zaidi Afrika Kaskazini.
Sasa kocha huyo atakuwa na kibarua kizito huko Casablanca ambacho anakabiliwa nacho kurudia mafanikio aliyoyapata Tanzania na kuirejesha Raja kwenye kiwango chake.
Fadlu ameachana na miamba hiyo ikiwa nafasi ya tano kwenye msimamo wa Ligi Kuu Morocco maarufu kama Batola Pro wakiwa na pointi 42 wapo nyuma ya vinara Fez kwa tofauti ya pointi mbili.