Mafanikio ya NSSF ndani ya siku 100 za Rais Samia
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Samia Suluhu Hassan.
Ndani ya siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Samia Suluhu Hassan, Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umepiga hatua kubwa na ya kihistoria kwa kuzindua mpango maalum wa uchangiaji wa hiari kwa wananchi waliojiajiri uitwao Skimu ya Hifadhi (Hifadhi Scheme). Mpango huu unatarajiwa kufikia mamilioni ya Watanzania wanaoweza kuchangia lakini walikuwa nje ya mfumo wa Hifadhi ya Jamii.
Uzinduzi wa Mpango huo ulifanywa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Sangu (Mb), Februari 9, 2026 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC).
Mpango huu ni sehemu ya utekelezaji wa hatua muhimu katika maboresho ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii ndani ya siku 100 tangu kuapishwa kwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan, Novemba 3, 2025. Aidha, hatua hii ni sehemu ya mafanikio makubwa katika kutekeleza ahadi za Muhula wa pili wa Serikali ya awamu ya sita kwa wananchi.
Waliojiajiri kujumuishwa katika mfumo rasmi
Kwa miaka mingi, zaidi ya asilimia 80 ya nguvu kazi ya Taifa, hususan wananchi waliojiajiri, wamekuwa nje ya mfumo wa hifadhi ya jamii na hivyo kukosa kinga dhidi ya majanga kama uzee, ulemavu, kifo, upotevu wa kipato au magonjwa yanayoweza kupunguza uwezo wa kufanya kazi. Kuzinduliwa kwa mpango wa Skimu ya Hifadhi kwa wananchi waliojiajiri na wanaoweza kuchangia kunaziba pengo hilo la kihistoria.
Aidha, mpango huo unatekeleza moja kwa moja Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii kwa kupanua ushiriki wa wananchi katika mfumo ya hifadhi ya jamii na kuhakikisha Watanzania wote waliopo katika sekta ya umma, sekta binafsi na waliojiajiri wanapata fursa sawa ya kujiunga, kuchangia na kunufaika na mafao ya hifadhi ya jamii.
Skimu ya Hifadhi (Hifadhi Scheme) ni nini?
Skimu ya Hifadhi ni mpango wa uchangiaji wa hiari unaolenga wananchi waliojiajiri, wakiwemo wakulima, wafugaji, wavuvi, wachimbaji wadogo wa madini, wasanii, machinga, waendesha bodaboda, wajasiriamali wadogo na wa kati pamoja na makundi mengine.
Kupitia mpango huu, wananchi wanaojiunga na kuchangia watanufaika na mafao ya pensheni ya uzee, pensheni ya ulemavu na pensheni ya warithi. Vilevile, watanufaika na mafao mengine ya muda mfupi yakiwemo mafao ya matibabu, mafao ya uzazi pamoja na huduma nyingine zinazotolewa na NSSF.
Mpango huu unamuwezesha mwananchi kujiandikisha bila gharama yoyote. Pia anatakiwa awe Mtanzania na mkazi wa Tanzania Bara, aliye na umri kati ya miaka 15 hadi 70 na asiwe mwanachama wa mifuko mingine inayotoa mafao ya hifadhi ya jamii kwa sasa.
Kiwango cha chini cha uchangiaji ni Sh 30,000 kwa mwezi kwa mwanachama mmoja ambapo atapata mafao yote ya msingi ikiwa ni pamoja na huduma za matibabu. Aidha, kiwango cha chini cha uchangiaji kwa mwezi ni Sh 52,200 kwa mwanachama, mwenza wake na watoto wasiozidi wanne.
Mwanachama anayeweza kuchangia kiwango cha juu anashauriwa afanye hivyo kwani mafao huongezeka kwa kadiri michango anayochangia mwanachama kwenye mfuko inavyozidi kuongezeka.
“Kivutio kikubwa cha skimu hii ni namna inavyoweza kuwajumuisha wananchi mbalimbali kwenye uchangiaji kwa kuzingatia hali halisi ya vipato vyao, ambapo mwanachama anaweza kuchangia kwa siku, wiki, mwezi au msimu kulingana na uwezo wake. Mwananchi pia anaweza kuwasilisha michango kwa njia anayoipenda na rahisi kwake ikiwa ni pamoja na kupitia simu ya mkononi popote alipo,” alisema Bw. Masha Mshomba, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF.
Pamoja na uzinduzi wa Skimu ya Hifadhi, mfuko unaendelea kutoa elimu na hamasa kwa Watanzania waliojiajiri ili wajisajili na kuchangia kwenye skimu hii muhimu. Wanachama wa Skimu ya Hifadhi walikuwa 509,839 hadi kufikia mwishoni mwa Februari 2026. Kama ilivyoelezwa awali, lengo la mpango huu ni kuwafikia wananchi wote waliojiajiri na wanaoweza kuchangia.
Serikali yaendelea kufanya maboresho katika sekta ya hifadhi ya jamii
Pamoja na uzinduzi wa mfumo wa Skimu ya Hifadhi kwa Wananchi waliojiajiri ndani ya Siku 100 tangu kuapishwa kwa Rais Samia, kwa mujibu wa takwimu za mfuko, hadi mwishoni mwa Desemba, 2025, thamani ya NSSF imeongezeka na kufika zaidi ya Sh 10.4 trilioni, hatua inayoashiria ongezeko la uwezo wa kifedha na uendelevu wa mfuko.
Ukuaji huu wa mfuko unaendelea kujenga imani ya wanachama kuhusu uimara wa mfuko na uwezo wake wa kutekeleza majukumu ya msingi ikiwa ni pamoja na ulipaji wa mafao. Sababu kubwa iliyochangia ukuaji huo ni maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya awamu ya sita katika mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji nchini. Maboresho haya yanachangia kwa kiasi kikubwa kwenye ongezeko la ajira, wanachama, michango, mapato ya uwekezaji na hivyo ukuaji wa mfuko.
Sambamba na mafanikio hayo, huduma za mafao zimeboreshwa ambapo kuanzia Februari 2026 wategemezi wa mwanachama walio na umri zaidi ya miaka 18 (au 21 kwa wanaosoma) sasa wananufaika na malipo ya mkupuo maalum pale mzazi mwanachama anapofariki, tofauti na awali ambapo hawakunufaika na mafao hayo.
Aidha, kuanzia Februari 2026 mwanachama aliyepoteza ajira na mwenye michango pungufu ya miezi 180 sasa anaweza kulipwa mafao yake yote kwa mkupuo (endapo ataridhia) baada ya miezi mitatu (siku 90) tangu kuachishwa kazi, tofauti na awali ambapo ilimlazimu kusubiri kwa kipindi kisichopungua miezi 24 (miaka miwili) kabla ya kulipwa mafao yake yote.
Mafanikio ya uwekezaji MkulaziMbali na mafanikio yaliyopatikana ndani ya siku 100 katika maboresho ya moja kwa moja ya sekta ya hifadhi ya jamii, Serikali kupitia NSSF na Jeshi la Magereza, imeendelea kuimarisha uwekezaji wa kimkakati katika kiwanda cha sukari cha Mkulazi. Tunafahamu kuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan alizindua rasmi kiwanda cha sukari cha Mkulazi Agosti 7, 2024 baada ya kuanza uzalishaji wa sukari ya majumbani Julai mwaka huo.
Ndani ya kipindi cha siku 100 cha Muhula wa pili wa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan, tayari kiwanda kimeanza kuzalisha sukari kwa matumizi ya viwandani (white sugar). Hadi kufikia mwishoni mwa Februari 2026, kiwanda kimeweza kuzalisha ajira za moja kwa moja 2,172 na zisizo za moja kwa moja 8,000 na kufanya jumla ya ajira zilizozalishwa kufikia 10,172.
Mbali na kiwanda kuzalisha ajira, wakulima wa maeneo jirani wanapata nafasi ya kulima miwa na kuiuza kiwandani, jambo linalochangia kwa kiasi kikubwa kuwaongezea kipato, kuboresha maisha yao na kukuza uchumi wa maeneo jirani, mkoa pamoja Taifa kwa ujumla.
Hadi kufikia mwishoni mwa Februari 2026, kiwanda kimezalisha zaidi ya tani 45,594 za sukari ya majumbani na viwandani. Mbali na kiwanda kuzalisha sukari kwa ajili ya matumizi ya nyumbani (brown sugar), kiwanda hiki ni cha kipekee na cha kwanza nchini kuzalisha sukari kwa matumizi ya viwandani (white sugar).
Kiwanda hiki pia kina uwezo wa kuzalisha megawati 15 za umeme, ambapo megawati saba zitaingizwa kwenye gridi ya Taifa kupitia kituo cha Msamvu mkoani Morogoro. Megawati nane zilizobaki ni kwa matumizi ya Kiwanda na shughuli nyingine kwenye mradi.
Mtazamo wa wananchi na mwelekeo wa siku 100
Baadhi ya wananchi waliojiajiri wameupokea mpango wa Skimu ya Hifadhi kwa matumaini makubwa na wameelezea jinsi unavyotoa fursa ya kujiwekea akiba ya uzeeni pamoja na kuwa na uhakika wa maisha ya sasa na ya baadaye kutokana na uwepo wa kinga dhidi ya majanga mbalimbali yakiwemo ya upotevu wa kipato na gharama kubwa za huduma za afya.
Wananchi hao pia wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika miradi inayogusa maisha yao moja kwa moja, ikiwemo mradi wa kiwanda cha sukari Mkulazi. Wamevutiwa mno na mchango wa kiwanda hiki katika kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja, jamii na Taifa kwa ujumla kupitia ongezeko la ajira, uzalishaji na fursa za biashara.
Aidha, wametoa shukrani kwa Serikali kwa maboresho ya kanuni za mafao, wakitaja kuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha ustawi wa wanachama na wategemezi wao.
Wataalamu wa masuala ya kijamii wanaeleza kuwa ujumuishaji wa wananchi waliojiajiri katika mifumo ya hifadhi ya jamii ni mkakati muhimu unaowajengea wananchi utamaduni wa kujiwekea akiba, kuondoa umaskini, kuchangia katika ustawi wa uchumi na kuboresha maisha kwa ujumla.
Uzinduzi wa Skimu ya Hifadhi na sera ya Taifa ya kinga ya jamii, maboresho mbalimbali yaliyofanyika pamoja na mafanikio yaliyopatikana ndani ya siku 100 za uongozi wa Rais Dk Samia Suluhu Hassan yanaonesha dhamira ya Serikali katika kuimarisha ustawi wa wananchi kupitia mfumo jumuishi wa hifadhi ya jamii kwa wote. Hatua hizi zinaweka msingi wa kupanua wigo wa kinga ya jamii, kuondoa umaskini, kuimarisha ustawi wa wananchi na kuhakikisha hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma tunapoendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.