Majina ya maeneo Zanzibar yanavyoacha watu midomo wazi
Mwonekano wa maghorofa katika eneo maarufu la Michenzani. Maghorofa hayo ni sehemu ya urithi wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Sheikh Abeid Amani Karume. Picha na Jesse Mikofu
Zanzibar ina simulizi na historia inayoweza kumvuta yeyote anayeisikia. Sio simulizi za masaibu ya historia ya siasa kwa wakazi wa kisiwa hicho kikubwa zaidi katika Bahari ya Hindi, lakini hata katika nyanja nyingine ikiwamo ya maendeleo ya makazi.
Kwa pamoja, visiwa vya Unguja na Pemba vinavyounda Zanzibar, vina utamaduni wa kipekee wa utoaji majina kwa maeneo yake. Kwa anayesikia majina hayo kwa mara ya kwanza, ni rahisi kupatwa na mshangao na pengine kujiuliza maana ya majina hayo.
Hebu pata picha unaposikia kwa mara ya kwanza ufundi uliotumika wa kupata majina ya maeneo kama Mchambawima, Mfereji Maringo, Jambiani, Kibanda maiti, Kaburi Kikombe, Chokocho, Mangapwani, Makunduchi,Saateni, Kijito upele, Bububu, Mlandege na mengineyo.
Ni majina yanayomvutia msikilizaji kutaka kujua maana yake. Huu ndio utamu wa utamaduni wa majina ya maeneo katika visiwa vingi ambavyo pia vina sifa ya kutumia miti kuyapa majina maeneo yake.
Zanzibar imejaa majina kama Mfenesini, Mkunguni, Miembeni, Kikwajuni, Mtundani, Michenzani, Migombani, Mtendeni, Misufini, Mkunazini na mengineyo.
Hata hivyo, mti uliotia fora zaidi kutumika ni mwembe, kwani umekuwa ukitumika sambamba na majina mbalimbali kama vile Mwembeshauri, Mwembatanga, Mwembenjugu, Mwembebeni, Mwembeladu, Mwembe kisonge, Mwembe mchomeke, Mwembemimba, Mwembe makumbi, Mwembe matarumbeta.
Lakini pia upo mti wa mbuyu wenye maeneo kama Mbuyu kidambwita, Mbuyu pacha na Mbuyu taifa.
Zanzibar pia tajiri wa maeneo yanayotokana na watu. Mifano ya maeneo hayo na watu husika kwenye mabano ni Kwahani (Ali Hani), Kwaalimsha (Ali Mcha), Kwasharifmsa (Sharifu Musa), Kwaalinatoo (Ali Natoo)
Makala haya kwa kurejea vyanzo mbalimbali, yanaangazia asili na historia ya baadhi ya majina ya maeneo maarufu kisiwani humo.
Bububu
Wengi hawajui kama Zanzibara hasa Unguja iliwahi kuwa na usafiri wa reli iliyojengwa mwaka 1905. Sauti na mlio wa treni hiyo ilipokuwa ikipita ikazaa jina bububu.
Barabara katika eneo la Bububu.
Hivyo bububu ni tanakali sauti yaani jina linalotokana na sauti ya kitu. Kama ilivyo sauti nyau kupewa paka/ nyau, ndivyo sauti ile ya treni ikipita relini bu-bu-bu ilivyozaa jina la eneo Bububu.
Mangapwani
Ni jina linalomaanisha pwani/ ufukwe wa mmanga au mwarabu. Eneo hilo kwa kuwa ni la pwani na lilikuwa likikaliwa na Wamanga yaani Waarabu, wazazi wa Kiafrika walikuwa wakiwakataza watoto wao kwenda kucheza maeneo ya pwan, wakiwaambia kuna Wamanga pwani, hivyo neno Mangapwani likazaliwa kumaanisha pwani ya Wamanga/ Waarabu.
Uzini
Inasemekana kuwa huko zamani wakazi wa hapo walitaka kulinda eneo lao, wakachimba mtaro kuzunguka eneo zima na kuweka uzi ndani ya mtaro huo kama ishara ya dawa ya kutambika.
Ikawa watu wakitaka kwenda hapo wanasema wanakwenda Uzini, huo ukawa mwanzo wa jina Uzini.
Mwembemchomeke
Nilisema awali kuwa wakazi wa Zanzibar walitumia utundi na ustadi wa hali ya juu kuyapa majina maeneo hayo. Moja ya jina ni mwembemchomeke lililotumiwa kama tafsida ya kuficha hali matendo ya utusitusi yaliyokuwa yakifanyika eneo hilo.
Mwonekano wa sasa wa eneo la Michenzani.
Simulizi zinaonyesha kuwa eneo hilo lilikuwa na matukio mengi ya ubakaji na kwa kupunguza ukali wa lugha, wenyeji wakapaita hapo Mwembe mchomeke.
Kibanda maiti
Ni eneo lililopo Unguja shehia ya Nyerere. Jina hilo limetokana na awali eneo hilo kuwa na kibanda kilichokuwa kikitumika kuoshea maiti.
Kisiwa Ndui
Ni mahala ambapo simulizi zinaeleza kuwa watu waliokuwa na ugonjwa wa ndui walihifadhiwa.
Mchambawima
Ustadi mwingine wa lugha kwa Wazanzibari unajionyesha katika jina la Mchamba wima. Kilugha kuchamba ni kujisafisha hasa kwa kutumia maji, pindi mtu anapotoka kujisaidia tena akiwa amechuchumaa.
Sasa simulizi zinaonyesha kuwa eneo hili lilikuwa na maji mengi hivyo kuwalazimu wapita njia kukunja nguo zao wanapopita
Kitendo cha kukunja nguo hali ya kuwa wamesimama kikafananishwa na mtu aliyevua nguo na kuchamba akiwa amesimama.
Chuini
Inaelezwa kuwa eneo hilo zamani kulikuwa na bustani na jengo lililokuwa likifuga wanyama wakiwamo chui.
Unadhani ni majina haya tu yanayowacha watu midomo wazi? La hasha! Yako mengi sana. Mwananchi tumeanza, wengine wanaweza kuchimba zaidi kuhusu utamaduni huu wa utoaji majina katika visiwa hivi vya karafuu.