Mwanafunzi UDSM apelekwa kituo kikuu cha polisi

Muktasari:

Alikamatwa na polisi jana na kuachiwa kwa dhamana akituhumiwa kusambaza picha kuonyesha nyufa kwenye majengo ya hosteli za UDSM.

Dar es Salaam. Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Kumbusho Dawson amehamishiwa Kituo Kikuu cha Polisi akitokea Oysterbay alikokwenda kuripoti.

Dawson alikwenda kuripoti Kituo cha Polisi Oysterbay leo Jumanne Desemba 5,2017 baada ya kuachiwa kwa dhamana jana usiku.

Mwanafunzi huyo ambaye ni mbunge wa serikali ya wanafunzi (Daruso) jana Jumatatu Desemba 4,2017 mchana alikamatwa na polisi akituhumiwa kusambaza picha kuonyesha nyufa kwenye majengo ya hosteli za UDSM.

Akizungumza na MCL Digital Makamu wa Rais wa Daruso, Anastazia Anthony alisema Dawson alikamatwa saa saba mchana na kupelekwa kituo cha polisi cha Chuo Kikuu kwa ajili ya kuhojiwa lakini ilipofika saa tisa alasiri polisi walisema hawana uwezo wa kumuhoji hivyo walimpeleka Oysterbay.