Dar yajipanga dhidi ya uhaba wa walimu wa sayansi

Muktasari:

  • Walimu hao licha ya kushika chaki kwa miaka zaidi ya 30 na kulipwa mafao yao na kiinua mgongo, bado ujuzi wao unahitajika kwa kuwa hauzeeki.

Wahenga waliwahi kusema: ‘ujuzi hauzeeki’. Kauli hii imewasukuma viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam kutangaza ajira za muda kwa walimu wastaafu wa masomo ya sayansi.

Walimu hao licha ya kushika chaki kwa miaka zaidi ya 30 na kulipwa mafao yao na kiinua mgongo, bado ujuzi wao unahitajika kwa kuwa hauzeeki.

Hatua hiyo imechukuliwa ili kukabiliana na tatizo la uhaba wa walimu wa masomo hayo ambao unazikabili shule nyingi za Serikali.

Ofisa elimu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Hamis Lissu anasema wamejipanga kukabiliana na tatizo hilo kwa njia mbili, ikiwamo ya kuwatumia wastaafu hao.

Njia nyingine anasema ni kuwatumia wahitimu wa masomo ya sayansi ya vyuo vikuuu pamoja na wahitimu wa kidato cha sita.

“Hii haimaanishi Serikali inatuachia jambo hili, bali wakati inaendelea kutuletea walimu wa sayansi na sisi tunaendelea kutafuta katika utaratibu tulioueleza hapo awali ili kuhakikisha wanafunzi wanafundishwa ipasavyo,” anasema.

Lissu anasema walimu wastaafu hawahitaji kibali kutoka ofisi ya kamishna wa elimu, bali watawaunganisha na wakurugenzi wa wilaya na manispaa waingie mkataba ili waendelee kutumia ujuzi wao.

“Kwa hao wastaafu tutaangalia yule anayeweza kuongea maneno yakaeleweka vizuri, hana matatizo makubwa ya kiafya tumeshatoa maelekezo kwa maofisa elimu ngazi ya manispaa tushirikiane katika kufanikisha hili,” anasema.

Anasema kuhusu kuwatumia wahitimu hao, tayari wamewaombea kibali kutoka ofisi ya kamishna wa elimu ili wapate leseni za kufundishia.

Anasema hatua inayofuata baada ya kuwapata walimu hao ni kukutana na wakurugenzi wa manispaa zote za Dar es Salaam na kujadiliana nao jinsi ya kuwalipa.

“Walimu hawa wote watakuwa wanalipwa posho na wakurugenzi, hivyo hii sio kwamba ni ajira ya kudumu, ni kibali cha kufundisha kwa kupitia leseni za miaka miwili,”anasema.

Anasisitiza: “ Baada ya hapo mwalimu au mhitimu huyo kama atapenda kuendelea na kazi ya ualimu nasi tukawa tumeridhika naye, tutamfanyia mpango akosome kozi ya mwaka mmoja ya stadhahada ya uzamili wa ualimu.”

Walimu wajitokeza

Fortnatus Kagoro ni Ofisa elimu taaluma wa mkoa huo, anaeleza tayari walimu wastaafu 49 wameshajitokeza kuomba nafasi ya kufundisha kwa mkataba kwa awamu ya kwanza.

“Idadi ya wastaafu waliojitokeza ni ndogo ikilinganishwa na ile ya vijana waliosomea masomo ya sayansi ambapo waliotuma maombi jumla yao ni 352 kati yao 100 wamesomea ualimu ambao wanasubiri ajira.

Baada ya kuwachuja, anasema o wamepatikana 99 hata hivyo kati yao ni 75 ndiyo wanaotarajiwa kunolewa kwa mafunzo ya awali.

‘’ Kuna sekondari 138 wakati idadi ya walimu ni 2313; kuna upungufu wa walimu 1323 wa sayansi, wakati kwa upande wa masomo ya sanaa kuna ziada ya walimu kama 880,’’ anasema.

Hatua hiyo ya Mkoa wa Dar es Salaam inasukumwa na maono ya Serikali kuu, ambayo yalibainishwa bungeni Juni 2016 na aliyekuwa Naibu Wizara wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Seleman Jaffo.

Alilieleza kwamba kutokana na uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi na Hisabati, serikali inaangalia namna ya kuwatumia walimu wastaafu wa masomo hayo kwa mkataba maalumu ili kupunguza tatizo hilo.

“Katika bajeti ya mwaka 2015/16 tuliona kwamba tunapaswa kuajiri walimu, lakini tutaenda mbali zaidi kwa walimu wa sayansi. Wapo wale waliostaafu lakini wana uwezo mzuri wa kufundisha tutaangalia jinsi ya kuwapa mikataba ili waweze kutumika,” alisema.

Hali ya walimu nchini

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako anataja takwimu za walimu waliopo nchini kwenye shule za sekondari za Serikali kuwa ni 88,999 ambapo kati yao 18,545 ni walimu wa sayansi na Hisabati. Anasema kuna upungufu wa walimu wa sayansi na Hisabati 22,460.

Pongezi za wadau

Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (Ten/Met), Cathleen Sekwao anapongeza hatua hiyo, akieleza kuwa ukosefu wa walimu wa sayansi ni changamoto, licha ya Serikali kutoa kipaumbele ufadhili kwa walimu wanafunzi wa masomo ya sayansi.

Sekwao ambaye amewahi kuwa mwalimu wa ufundi kwa miaka 23, anaeleza kuwa kuna changamoto nyingi kuhusu walimu na kwa kiasi kikubwa zinaathiri zaidi mchepuo wa masomo ya sayansi ikilinganishwa na michepuo mingine.

“Kuna mambo yanawakamisha walimu ikiwamo mazingira duni ya kazi ya walimu yanayowavunja moyo kufundisha. Pia, uoga wa wasichana kusomea masomo ya sayansi nayo ni changamoto ya aina yake, licha ya jitihada zinazofanywa na Serikali kutoa upendeleo kwa wanafunzi wa sayansi,’’ anasema na kuongeza:

“Maneno kwamba walimu ndiyo wanalipwa mshahara mdogo pia yanasababisha vijana wahitimu wa ualimu kukimbia fani, ingawa ukweli ni kwamba kuna tofauti ndogo na watumishi hasa wa sekta ya afya.’’