Eliuter: Viongozi Friends waliniwekea mizengwe

Muktasari:

  • Mpepo (20) ameichezea Prisons mechi saba na kufunga mabao matatu, likiwemo bao maarufu alilomfunga kipa wa Yanga, Youth Rostand wakati timu hizo zilipofungana bao 1-1.

Mshambuliaji Eliuter Mpepo amekuwa mchezaji muhimu kwenye kikosi cha Tanzania Prisons na ameonekana kutolewa macho na vigogo wa soka kutokana na uwezo wake katika ushambuliaji.

Mpepo (20) ameichezea Prisons mechi saba na kufunga mabao matatu, likiwemo bao maarufu alilomfunga kipa wa Yanga, Youth Rostand wakati timu hizo zilipofungana bao 1-1.

Kabla ya kutua Tanzania Prisons, mshambuliaji huyo amezichezea Kinyerezi United, Friends Rangers na Mbeya Kwanza.

Hata hivyo, Mpepo anasema hawezi kusahau mazingira aliyopitia akiwa Friends Rangers.

“Ulifika wakati nikaanza kuwaza kuachana na soka. Nilivyojiunga na Friends kuna baadhi ya viongozi walikuwa hawanipendi kabisa hivyo walinitengenezea zengwe kwa hata kupandikiza chuki kwa mashabiki,” anasema Mpepo..

“Kwa kweli walifanikiwa maana kila nilipokuwa ninaingia uwanjani nilikuwa ninazomewa. Nilishindwa kumudu hali ya kuzomewa hadi ikaanza kuathiri uwezo wangu wa kawaida uwanjani. Nilipiga moyo konde na kuushinda ule mtiani.”

Pamoja na kuonekana kuwa mmoja wa washambuliaji hatari kwa sasa, Mpepo anasema hana tatizo wala mapenzi kati ya Simba na Yanga kama ukitokea upande wowote kumwitaji atakuwa tayari kuusikiliza.

“Ninafanya kazi popote bila ya kuhofia chochote,” anasema.

“Ninaweza kucheza Simba na hata Yanga kama wakinihitaji. Ninamshukuru sana kocha wangu wa Tanzania Prisons, Abdallah Mohammed kwa kuniamini na kunipa nafasi.”

Mbali na kocha wake, Mpepo aliwataja watu wengine ambao wamechangia kukua kwake kisoka ambao ni Kivunje, Olenjo, Mwenjala na Henry Mzozo.

“Kivunje alinifundisha mpira Kinyerezi pia nilikuwa nikipewa sana moyo wakati napitia magumu na familia ya Mr Mwambete, Nguvumali, Shiraz Batchu na kaka yangu Justin, bila hao ingekuwa ngumu kufika hapa nilipo,” anasema.

Hata hivyo, mshambuliaji huyo mwenye uwezo wa kucheza nafasi zote za ushambuliaji, alisema kama si soka anaamini kuwa kazi ya ununuzi na ugavi ingemtoa kimaisha kwa sababu ni kazi ambayo ameisomea.