Jadili unachotaka kulipwa na mwajiri

Muktasari:

Watu wengi hupumbazwa na furaha ya kupata ofa ya kazi waliyokua wanataka, kiasi cha kuwasababishia kukubali masharti yanayokuja na ofa bila kuyaafiki.

Huwezi kupata malipo unayostahili bila kujadili mshahara.

Watu wengi hupumbazwa na furaha ya kupata ofa ya kazi waliyokua wanataka, kiasi cha kuwasababishia kukubali masharti yanayokuja na ofa bila kuyaafiki.

Unatakiwa ukumbuke kupata ofa ya kazi sio mwisho wa mahojiano na badala yake unaingia kwenye sehemu ngumu zaidi ambayo ni makubaliano kuhusu malipo ya mshahara na marupurupu mengine.

Unaweza kuwaza kwamba labda mwajiri wako atabadili mawazo ukiomba fedha zaidi, au usubiri mpaka uthibitishe uwezo wako ndio uombe mshahara unaotaka.

Lakini kupata mshahara unaotaka, kunategemea kwa kiwango kikubwa na jinsi unavyojiamini. Kama unajua ujuzi utakaoleta kwenye kampuni na thamani yake, lazima uwasilishe pendekezo zuri kuhusu malipo yako.

Hata hivyo, zaidi ya kujiamini kuna njia unazoweza kutumia kuafikiana mshahara baada ya kupata ofa ya kazi.

Fanya utafiti katika sekta

Kufanya utafiti wa kiwango cha mshahara kilichopo kwenye sekta ya kazi unayoomba, ni suala muhimu kabla ya kwenda kufanya usaili wa kazi.

Hii ni kwa sababu waajiri wengi watakuuliza kuhusu mshahara unaotegemea kulipwa.

Uliza kwa jamaa na marafiki au fanya utafiti mtandaoni na ukishajua kiwango, ongeza asilimia 30 ili upate nafasi ya kufanya maelewano na wahusika.

Jadili bima, mifuko ya jamii na faida nyingine. Ukishapata ofa ya kazi mwajiri wako atakupa mgawanyo wa mshahara wako, michango na bonasi. Akishafanya hivi sasa ni zamu yako kuleta mahitaji yako, usianze na mshahara au bonasi badala yake uliza maswali kama mchango wako katika mfuko wa jamii. Asilimia ngapi ya mshahara itatumika na mwajiri atachangia kiasi gani.

Aina ya bima ya afya, gharama yake na kama utarudishiwa gharama za usafiri kwenda kwenye mikutano ya kikazi.

Useme nini wakati wa maafikiano ya mshahara?

Kusaidia kufikisha maombi yako kwa urahisi, unaweza kusema kitu kama; “Nina furaha ya dhati kuanza kufanya kazi na nyinyi, Ninaamini nitaleta mchango na mafanikio makubwa hapa. Nimetathmini ofa yenu ya Sh2,000,000 lakini kutokana na uzoefu wangu wa miaka mitano katika sekta hii

na wateja ambao nitawaleta hapa, nilikua nategemea ofa ya Sh3,500,000.’’

Kumbuka mwajiri wako anategemea majadiliano haya, hivyo kistaaarabu sisitiza kuhusu mshahara uliokuwa unategemea. Atakapokupa jibu kwamba hawezi kuongeza mshahara na ukajiridhisha kwamba hawezi, omba muda wa kufikiria.

Usisahau kuhusu bonasi

Ukiondoa mshahara, unaweza pia kujadiliana na mwajiri kuhusu bonasi. Tumia utaratibu kama uliotumia wakati mnaelewana kuhusu mshahara. Hapa kumbuka kuuliza bonasi yako itakokotolewa vipi? Nani atakuwa na wajibu wa kutathmini na kuamua bonasi yako na utaipata kila baada ya muda gani?

Usipouliza hutojua

Watanzania ni watu wastaarabu, wengi tunaona aibu kuongelea ni fedha kiasi gani tunahisi tunafaa kulipwa. Lakini hakuna ambaye atakataa kulipwa zaidi ya anacholipwa sasa.

Kwa hiyo, njia bora ya kupata fedha zaidi kutoka kwa mwajiri wako ni kumwambia kiasi unachotamani kutokana na majukumu anayotarajia kukupa.

Makala haya yameandaliwa kwa hisani ya shirika la Brighter Monday. www.brightermonday.co.tz

Mak.brightermonday.co.tz