Kuna tofauti kati ya msanii anayetaka kurudi na yule anayetaka kuweka heshima kwenye gemu

Muktasari:

Nyakati zimebadilika na muziki haukubaki nyuma. Bongo Fleva kama kawaida huwa inasukumwa na upepo. Nakumbuka kuna wakati kwaito na sasa tumetekwa na Nigeria.

Miaka 10 nyuma niliwahi kuwaambia marafiki zangu kuwa nitakuwa shabiki wa mwanamuziki Lady Jay Dee siku zote hata kama angeacha kuimba wakati ule.

Nakumbuka nilikuwa nasikiliza nyimbo zake kama Binti, Rafiki wa Mashaka, Mawazo, Umuhimu Wako, Siri Yangu, makini na nyingine nyingi ambazo vijana waliozaliwa enzi za utawala wa Rais Benjamin Mkapa hawazijui.

Nyakati zimebadilika na muziki haukubaki nyuma. Bongo Fleva kama kawaida huwa inasukumwa na upepo. Nakumbuka kuna wakati kwaito na sasa tumetekwa na Nigeria.

Kuna wanamuziki wanaibuka na kupotea. Wanapendwa, wanatengeneza mamilioni ya fedha na baadaye wanapotea kabisa. Lakini Lady Jay Dee yupo na heshima yake ipo palepale.

Siyo kwamba amependelewa, lah hasha, isipokuwa ipo siri moja ambayo wanamuzii wengi wangeijua kamwe wasiongepotea kwenye muziki.

Tatizo huwa linakuja pale mwanamuziki anapoondoka kwenye chati halafu akawa hana kitu na kutaka kufanya muziki wa ushindani.

Kumbuka kuna mahali ukifika unabaki kwenye ligi yako mwenyewe. Unaimba kujenga heshima na kilinda hadhi lakini siyo kushindana na wengine. Mashabiki wanakiburi sana, hasa wanapojua jamaa anataka kurudi. Wanasikiliza wimbo kwa kulinganisha.

Kuna wasanii unaona wanavyohangaika kutoka tena, lakini wanarudi kwa staili zilezile za zamani wakati muziki umeshapiga hatua umekwenda mbali.

Ukifanya muziki ‘kidon’ kama Lady Jay Dee, AY, MwanaFA, Profesa Jay na wengine inakulindia heshima yako na watu wanasikiliza au kununua kazi kama legend. Hushindani na mtu wala hushindanii ligi iliyopo.

Wanamuziki wajifunze kuwa kuna wakati hawatatakiwa kufanya muziki wa njaa. Ifike mahali jina lako liuze kazi. Yaani unaamka asubuhi unatupia sokoni albamu ya kushtukiza na ikifika saa saba mchana umemaliza mzigo.

Lady Jay Dee sasa hivi akifanya shoo wala hatumii nguvu nyingi kujitangaza kwa sababu amejijengea heshima na mashabiki wa kudumu.

Asikwambie mtu njaa mbaya na inapunguza uwezo wa kufikiri. Ukiwa na mkwanja ni rahisi pia kufanya kazi inayoendana na hadhi ya jina lako ndio maana unaona leo wasanii wanaruka viwanja kwenda kutengeneza kazi nzuri.

Muhimu wasanii wajijengee heshima na wafanye uwekezaji kwenye bisahara nyingine ili waache kuimba kwa sababu ya njaa. Watakesha.