Kunywa juisi ya embe uone vizuri, maganda kwa ngozi yako

Muktasari:

Tunda hili, licha ya ladha yake nzuri pamoja na utamu wake, linaweza kutumika kwenye milo yote ya siku kwa familia nzima.

Matunda ni miongoni mwa virutubisho muhimu kwa binadamu kwa sababu yana viinilishe vingi ambavyo husaidia mwili kuwa na afya bora.

Tunda hili, licha ya ladha yake nzuri pamoja na utamu wake, linaweza kutumika kwenye milo yote ya siku kwa familia nzima.

Ulaji wa mara kwa mara wa tunda hilo husaidia kupunguza kiwango cha asidi mwilini, kuboresha mmeng’enyo wa chakula na kurekebisha kiwango cha insulin. Husaidia kusafisha damu pia, kuimarisha muonekano wa ngozi, kuzuia saratani na kuimarisha kinga ya mwili.

Vilevile, husaidia kutibu kiharusi, hupunguza kiwango cha lehemu na husaidia kupunguza mawe kwenye figo. Faida nyingine ni kuongeza madini ya chuma kwa wajawazito, kupunguza uzito na kulinda macho dhidi ya magonjwa.

Unywaji wa juisi yake kila siku husaidia kuleta uoni mzuri kwa sababu juisi hiyo ina vitamini A ambayo huimarisha afya ya macho na kuwasaidia wale wenye macho makavu au wasioona vizuri hasa usiku, night blindness.

Hata hivyo, juisi ya embe inapotumika bila kuwekwa sukari ni nzuri kwa watu wenye kisukari kwa sababu husaidia kurekebisha tatizo hilo pamoja na kurekebisha mapigo ya moyo kuwa sawa na kuondoa sumu mwilini.

Vile vile juisi hii inasifika kwa kuimarisha mmeng’enyo wa chakula na huondoa ukosefu wa choo ikichanganywa na nanasi.

Licha ya vitamini A, juisi ya embe ina vitamini C pamoja na carotenoids ambazo husaidia kuimarisha kinga za mwili hivyo kuwafaa zaidi wenye upungufu wa kinga hizo, wanaonyemelewa na magonjwa au wenye maradhi ya muda mrefu mfano pumu.

Embe linafaida kubwa katika afya ya ngozi kwani ukipaka maganda ya embe usoni na kukaa nayo kwa muda usiopungua dakika kumi kisha ukanawa kwa maji yanayotiririka au yale yanayotoka bombani husaidia kuifanya ionekane nzuri.

Wataalamu wa masuala ya urembo hutumia maganda haya kuondoa kero nyinginezo zinazojitokeza na kuharibu muonekano wa ngozi kama vile kutibu chunusi.