Nchama The Best : Kutoka Mwanza mpaka Dar

Muktasari:

Amezaliwa jijini Mwanza katika Mtaa wa Bugarika. Ni mtaa ambao una sifa za kipekee, baadhi ya sifa zake ni upikaji wa Pombe haramu.

       Nchama The Best, si jina geni haswa kwa wale wapenzi wa muziki wa Hip Hop. Jina lake halisi Nchama Anthony (23).

Amezaliwa jijini Mwanza katika Mtaa wa Bugarika. Ni mtaa ambao una sifa za kipekee, baadhi ya sifa zake ni upikaji wa Pombe haramu.

“Mimi ni mtoto wa pili kati ya sita kwenye familia ya Mzee Anthony Rocket. Kati yao, ni mimi tu ambaye imebarikiwa au mwenye kipaji cha sanaa ya uimbaji,” anasema.

Anasema kama wasanii wengine, amaepata taabu sana kabla ya kufika hapo alipo. Amefanya nyimbo nyingi tu ambazo hazikuweza kupata nafasi au kupendwa.

“Nimekuwa kwenye hii gemu miaka mingi. Ni bidii na kipaji changu ndiyo vigezo ambavyo vimeniweka hadi sasa hivi,” anasema Nchama.

Baadhi ya nyimbo zake ni pamoja na Kwa Ajili Yako, Soja, Nastrago na Waiter Leta.

Ilikuaje hadi ukaanza kuimba?

Anaeleza kwamba yeye amelelewa katika familia ya kipato cha chini na siku zote katika kile ambacho alikusudia kukifanya amekuwa akikifanya kwa bidii akikumbuka hali halisi ya maisha ya pale nyumbani.

Bugarika ni mtaa wa aina nyingi za maisha na hivyo mtu asipokuwa makini ni rahisi sana kujikuta angle nyingine kinyume na matarajio.

“Niliamua kuingilia fani hii, kwanza kama kipaji change lakini pia kutafuta riziki. Na namshukuru Mungu hali yangu ya maisha inaendelea kuimarika japo kwa mwendo wa wastani,” anaeleza Nchama.

Nchama kama vijana wengi wa Bugarika, aliwahi kuathirika na pombe kali maarufu kama ‘gongo’. Pombe hii ilimsababishia madhara kiafya maana kila alipoitumia, aliugua hususan tumbo.

“Kuna baadhi ya vitu mtu anajikuta amejiingiza pasipo hata yeye mwenyewe kujua. Nilikuwa mnywaji wa gongo kwa siku nyingi tu lakini namshukuru Mungu aliniepusha na hali hiyo na kwa sasa nipo shwari nakomaa,” anasema.

Alifanikiwa kuacha

Nchama The Best anasema kwamba licha ya kuwa na marafiki wengi wa kitaa ambao ni walevi na watumiaji wa dawa za kulevya, moyoni alitambua kwamba alikuwa na jukumu la kulitekeleza maishani… muziki.

“Haikuwa rahisi kuwakwepa ‘wanangu’ marafiki na kuanza kufanya mambo yangu kwa ajili ya manufaa yangu na jamii inayonizunguka,” Nchama.

Mwaka 2012 aliamua kutupia ndoano yake ili kuona kama angeambulia hata kidagaa tu.

“Sigara ya SM, waliandaa mashindano maalum ambayo waliyaita ‘Str8t Free Style Competion’, nilibahatika kuwa mshindi wa pili. Wlikuwa wameahidi kwamba mshindi wa kwanza na wa pili wangeweza kupata ufadhili wa kurekodi nyimbo kadhaa Dar Es Salaam ingawa haikuwezekana,” anabainisha.

Kampuni hiyo hiyo ilirejea mwaka uliofuata (2013), na kuandaa mashindano kama kawaida na kutoa ahadi zile zile. Awamu hiyo, Nchama The Best alifanikiwa kuibuka mshindi.

Mwaka 2016, Nchama The Best, aliweza kubahatika tena katika shindano la Super Nyota ambalo liliandaliwa na Clouds Media.

Ni hapa ambapo aliweza kudhihirisha uwezo wake wa kuchana na hivyo kuwa mmoja kati ya wasanii wa Mwanza waliokubalika kuwa sehemu ya burudani kwenye mzunguko wa Fiesta kwa udhamini wa Tigo.

“Hapa nilibahatika kwa mara ya kwanza kushiriki shoo ya watu wengi ambao iliofahamika kama Tigo Fiesta chini ya Clouds Media. Nilijiskia fahari sana na tangu hapo nilianza kuwa na ule ujasiri wa kupiga shoo kwa watu wengi,” Nchama.

Mwaka huu 2017, Nchama The Best pamoja na wasanii wachahche kutoka Mwanza, alibahatika kushiriki katika tamasha la Tigo Fiesta ambayo ilianzia mkoani Arusha na kufikia kikomo jijini Dar es salaam, siku chache zilizopita.

Anasema akiachilia mbali zile Ngoma zake za zamani, Nchama The Best kwa sasa anatamba na muziki wake ambao unapikwa na watu mbali mbali ambao ni wataalam wa siku nyingi katika kuhakikisha kwamba anakuwa sehemu nzuri.

Baadhi ya Ngoma zake kali ni pamoja na Tufanye Kesho ambayo amemshirikisha Dully Sykes, Kwa Muda na Wanangu.

Kwake yeye, kukacha utumiaji wa hgongo, ni mafanikio. Hakupelekwa ‘sober house’ kama wasanii wengine ila aliwahi kujitambua kwa kuzingatia mazingira ya nyumbani kwao, Bugarika.

“Kwa wale ambao waliwahi kuathirika na dawa za kulevya ikiwemo pombe, wanaelewa nnachoizungumzia. Kuacha tabia hizi ni kibarua kigumu sana, leo utaacha kesho utarudia. Lakini mimi niliamua na kusimama imara,” Nchama

Anasema licha ya kwamba hajafahamika kiviile, ni imani yake kwamba atatendelea kufanya vizuri ili muziki umlipe kama wenzake wakongwe wanavyofanya.

“Bidii na ari ya kutaka kufika mbali ndiyo silaha tu ya kufanya vizuri baada ya kujikita katika nidhamu,” anasema.