MBALAMWEZI YA KISWAHILI : Ninakwenda shule au ninakwenda shuleni?

Muktasari:

Tungo zifuatazo kimuundo zinalingana na tungo tajwa juu. Ebu tuziangalie na kuzichunguza: (i). Ninakwenda ofisi* (ii). Nipo kanisa.* Kwa mtumiaji wa Kiswahili aliyezoea kutamka ‘Ninakwenda shule’ au ‘Nipo chuo’ anaweza kuona kwamba matumizi hayo ni sahihi. 

 Imezoeleka kwa baadhi ya watumiaji wa Kiswahili kutumia tungo kama hizi: ‘Ninakwenda shule’, ‘Nipo chuo’, ‘Natoka hospitali’ na kadhalika.

Tungo zifuatazo kimuundo zinalingana na tungo tajwa juu. Ebu tuziangalie na kuzichunguza: (i). Ninakwenda ofisi* (ii). Nipo kanisa.* Kwa mtumiaji wa Kiswahili aliyezoea kutamka ‘Ninakwenda shule’ au ‘Nipo chuo’ anaweza kuona kwamba matumizi hayo ni sahihi. Kulingana na kanuni za lugha, tungo hizo si fasaha.

Maneno ‘shule’, ‘chuo’ na ‘hospitali’ ni nomino katika aina za maneno. Kulingana na taratibu za lugha, vitenzi ‘ninakwenda’, ‘nipo’ na ‘natoka’ katika muktadha huo havipaswi kufuatiwa na nomino kama ilivyo katika mifano hiyo hapo juu. Badala yake, vitenzi hivyo vinapaswa kufuatiwa na vielezi (vya mahali). Kwa sababu hiyo, tungo hizo zinapaswa kuwa ‘ninakwenda shuleni’, ‘nipo chuoni’ na ‘natoka hospitalini’.

Tukichunguza tungo namba (i) na namba (ii), tunaona kwamba tungo hizo zina makosa ya wazi ilhali zile za awali (ninakwenda shule, nipo chuo, nakwenda hospitali) ni vigumu kuona makosa hayo kwa kuwa watumiaji wengi wa Kiswahili wamekuwa wakizitumia na kuona kwamba ni sahihi. Kama ufasaha unavyokosekana katika tungo (i) na (ii) juu, ndivyo tungo hizi zinavyokosa ufasaha pia.

Sentensi (i) na (ii) kwa ufasaha zingepaswa kuwa: ‘Ninakwenda ofisini’ na ‘Nipo kanisani’.

Kulingana na uchunguzi mdogo uliofanywa na Mbalamwezi ya Kiswahili, watumiaji wengi wa lugha hususan wa maeneo ya mijini, hupenda kutumia lugha kwa namna hiyo (ninakwenda shule, nipo chuo na natoka hospitali), watumiaji wa Kiswahili wa Dar es Salaam na Pwani wakiongoza. Itambulike kwamba kufanya hivyo ni kukiuka kanuni za ufasaha wa lugha.

Aidha, kwa wale wanaotokea katika maeneo yasiyo ya mijini wao hawana shida katika hilo ingawaje wana namna yao ya kubananga katika muktadha huo. Kwa mfano, utasikia baadhi yao wakisema, “Nakwenda kanisanini”* badala ya “Nakwenda kanisani” au wengine husema “Nakwenda bustani”* badala ya “Nakwenda bustanini”. Jambo la msingi la kuzingatiwa katika muktadha kama huu ni kwamba mofimu ‘ni’ huongezwa kwenye nomino inayohusika ili kuunda kielezi kitakachoendana na kitenzi hicho.

Kwa hivyo, mwishoni mwa neno mathalani ‘bustani’ huongezwa ‘ni’ na kuwa ‘bustanini’. Aidha, kwa kuwa neno ‘kanisa’ ndiyo nomino, ‘ni’ huongezwa mbele ya nomino hiyo na kuunda neno ‘kanisani’ na siyo ‘kanisanini’ kama wengine walivyozoea kulitumia.

Pia, wapo watumiaji wengine wa lugha ambao badala ya kutumia ‘ni’ mwishoni mwa nomino husika, hutumia ‘kwa’ kwa lengo la kuonesha mahali ambapo tukio hutendeka. Kwa mfano, mtumiaji wa lugha huweza kusema, “Nakwenda kwa ofisi”. Matumizi ya ‘kwa’ katika muktadha huo hayaendani na taratibu za lugha. Mtumiaji huyu wa lugha kwa kuzingatia kanuni za lugha alipaswa kusema, “Nakwenda ofisini.” ‘Kwa’ hutumika ikiwa jina au cheo cha mtu kinahusika. Mathalani, “Nakwenda kwa mwalimu”

Aidha, yapo maneno ambayo watumiaji wa lugha huyatumia kwa makosa. Kwa mfano, neno ‘mchanga’ hutumika hivyo katika umoja na wingi. Baadhi ya watumiaji wa lugha wanapolitumia katika muktadha wa wingi hulitaja kama ‘michanga’. Utumiaji huo si fasaha. Maneno mengine yanayotumika visivyo ni ‘dazani’ badala ya ‘dazeni’ likiwa na maana ya ‘jumla ya vitu kumi na viwili’. Halikadhalika, neno ‘deksi’ hutumiwa kwa makosa badala ya ‘deski’likiwa na maana ya dawati.