Sifa muhimu kwa wahitimu wanaotafuta ajira

Muktasari:

Mazingira ya kufanyia kazi yanabadilika kwa haraka zama hizi za sayansi na teknolojia.


Mazingira ya kufanyia kazi yanabadilika kwa haraka zama hizi za sayansi na teknolojia.

Hali hii bila bila shaka inahitaji watu wanaoweza kwenda na mabadiliko hayo kwa kasi.

Watafuta ajira nao hawana budi kuyajua ya mabadiliko haya teknolojia na kisha kutafuta mbinu za kwenda nayo sambamba.

Huu siyo tena wakati wa kufanya vitu kizamani, unapaswa kutumia teknolojia kujiuza na kupata kile unachohitaji maishani.

Ili kujiweka katika nafasi nzuri katika soko la ajira na kurandana na hali halisi ya sasa, ni muhimu kwa wahitimu kuzingatia mambo kadhaa.

Uwezo wa kutumia zana za digitali

Vifaa vya digitali vimetengeneza nafasi ya watu kuingiliana na kuwa karibu zaidi na kupanua mianya ya ajira.

Katika dunia ya sasa, siyo lazima maombi ya kazi yafanywe kwa barua au siyo lazima kwa mtu kuhangaika na magazeti akitafuta ajira; haya yote sasa yanawezekana kwa kutumia njia za kisasa za vifaa vya kidigitali.

Kwa sasa sio uamuzi wako kuamua kujifunza komputa au la, bali ni lazima mno ili uweze kuendana na uhalisia wa dunia kiteknolojia. Siyo kwa kutafutia ajira, lakini hata kazi sasa zinafanywa kiteknolojia zaidi.

Uwezo wa kufanya kazi na kuwasiliana na watu

Huombi ajira ili uje kujifungi chumbani ukifanya kazi peke yako, ni lazima uchangamane na wenzako katika ofisi moja au taasisi. Kuwa karibu na wenzako kwa kushirikiana kuhusu mambo yote muhimu kwa manufaa ya ofisi. Hakikisha unawashirikisha taarifa au maarifa mapya kutoka mahali kwingine ili kwa pamoja muweze kufikisha malengo kusudiwa.

Uwezo wa kuwasiliana ni muhimu kwa mfanyakazi mpya, kwani utakuwezesha kuwasilisha mawazo yako na kuyafanya yaeleweke vyema na kutumiwa na timu yako. Hivyo jifunze kuja na mawazo makubwa zaidi na kuwasilisha kwa unadhifu.

Elimu ya ujasiriamali

Huhitaji kumiliki biashara yako ili uwe na uwezo wa kupata mawazo makubwa na mapya, bali kupitia mabadiliko ya kiteknolojia yanaweza kukusaidia kujitambua na kujua unachopaswa kukifanya.

Ukijituma na kuwa mbunifu, ni dhahiri kuwa fursa zaidi zitakufuata mikononi mwako. Elewa kuwa hivi sasa kampuni nyingi hazihitaji wahitimu bali watu walio tayari kusababisha mabadiliko chanya na endelevu.

Kampuni zinataka mawazo mapya na watu wenye mipango stahiki walio na uthubutu wa kutenda kwa kuwa tayari wana tabia za kijasiriamali ndani yao.

Fahamiana na watu wengi kibiashara

Kuwa na mtandao mkubwa ambao umeutengeneza ni muhimu sana katika utendaji wa kisasa, kwani licha ya kuwa na msaada katika kuboresha biashara mauzo au huduma pia itakuwezesha wewe kujifunza mambo mbalimbali na kujiongezea uelewa jambo ambalo lina umuhimu mkubwa.

Mtandao ulionao una nguvu kubwa katika masoko yako hivyo kabla hujapata kazi jitahidi kuwa na watu sahihi. Pia, ni muhimu kujifunza namna ya kuwalinda na kuutunza urafiki wako na watu wako muhimu.

Uwezo wa kuchambua na kung’amua taarifa

Kuwa na taarifa nyingi na sahihi ni jambo kubwa mno katika karne hii. Kuwa na taarifa nyingi na maarifa ya kutoosha kutakusaidia kufanya jambo lolote kwa usahihi wake.

Unapaswa kuwa mchambuzi wa kilaa taarifaa unayoipata katikaa vyanzo mbalimbali. Kuwa makini na taarifa unayoichagua katika kutekeleza majukumu yako.

Kumbuka nyakati za kufanya kazi bila mpangilio na kwa kubahatisha zilishapita miaka mingi.

Uwezo wa kufikiri kwa mapana na usahihi

Ubunifu unathaminiwa na kampuni nyingi duniani. Ubunifu ndicho kitu pekee kinachosababisha kampuni kubakia kileleni katika ushindani wa dunia kibiashara.

Hivyo ni jambo zuri kuwa na watu ambao husugua akili zao kwa kujua nini kifanyike kwa maendeleo chanya ya namna ya kuboresha kazi au bidhaa.

Uwezo wa kujifunza kila siku

Kwa kadri teknolojia inavyokua na kubadilika, ndivyo unavyotakiwa kuendana nayo kama unataka kufanikiwa. Fungua akili yako na jifunze kwa watu wengine.

Hivi sasa watu hawajifunzi tena wakiwa darasani, zana za Tehama kama zimerahisisha watu kujifunza mambo mbalimbali, hivyo huna sababu ya kutojifunza.

Uwezo wa kutatua matatizo

Katika ulimwengu unaobadilika kwa kasi, matatizo yanazaliwa kila kukicha na hakuna muda tena kumsubiri bosi kukuonyesha njia kama unakijua unachokifanya. Unatakiwa kuwa na uwezo kutambua matatizo na kuyatafutia ufumbuzi sanjari na kupendekeza nini kifanyike kwa haraka kadri matatio yalivyojitokeza.

Hii ina maana moja tu kuwa fikiria kwa njia yako kabla ya kulaumu. Wakati wote uwe mtu wa kuonyesha njia ya kutokea badala ya kukata tamaa.

Kama wewe ni mhitimu na unahitaji kufanya kazi ya ndoto yako ambayo umeisomea, hakikisha unajivika sifa hizi ili uwe mshindani wa kweli katika soko la ajira. Kumbuka kuna wengi wanatafuta kazi hiyohiyo unayoitafuta wewe.

Makala haya awali yalichapishwa katika tovuti ya Brighter Monday, ambayo ni tovuti namba moja ya ajira nchini.