Unique Band na mpango wa kulikamata soko la burudani

Muktasari:

Ni miezi miwili tangu kuanzishwa kwa kundi hili lakini umahiri wao katika kuimba na kupiga vyombo umewafanya wapewe kibali cha kutumbuiza kila mwisho wa wiki.

Ni vijana wanne  wasomi, wenye vipaji na ndoto za kufika mbali kupitia muziki wa kizazi kipya.

Wasanii wanne wanaunda kundi hilo ambao ni Herman Kibasso (Nicolass Nana), Rommy Romwad (Rommy The Base), Loyce Paul (Loichi) na Alex Exavery (Lexy Gitaa).

Vijana hao wanne wanapiga gitaa, kinanda na kuimba. Ukitaka kuujua umahiri wao tembelea Klabu ya Ground Zero iliyopo Kurasini jijini Dar es Salaam.

Kila siku ya Jumamosi, baada ya masomo ya wiki nzima hutumbuiza katika klabu hiyo.

Ni miezi miwili tangu kuanzishwa kwa kundi hili lakini umahiri wao katika kuimba na kupiga vyombo umewafanya wapewe kibali cha kutumbuiza kila mwisho wa wiki.

Meneja wa kundi hilo, Alex Exavery ‘Lexygitaa’ anasema lengo  la kuanzishwa kwa bendi yao ni kutaka kuonyesha mfano kwa kufanya kazi na watu kutoka sehemu yoyote duniani.

“Tunataka tuwe watu ambao tunaweza kufanya kazi na watu kutoka sehemu mbalimbali duniani, tuwe na vitu ambavyo watu wengine wameshindwa kuvifanya kwa mfano  hivi sasa tumeanzisha programu ya nyimbo mbalimbali za kigeni ikiwemo Kichina, Kijapani, Kikorea na Kiitaliano.” alisema Alex.

 Alisema lengo kubwa la kufanya hivyo ni kutaka kukusanya mashabiki kutoka sehemu mbalimbali na hata wageni watakapokuja kutoka nchi za nje basi bendi yao iwe moja kati ya wale watakaopewa kipaumbele katika kuwaburudisha  kwa lugha zao.

Alisema licha ya kufanya hivyo pia wao kama The Unique band wanafanya kazi sehemu yoyote ile ikiwa ni kwenye harusi,sherehe ya kuvalishwa pete,kuzaliwa.

Jinsi walivyokutana

Alex anasema yeye pamoja na Rommy wanasoma chuo kimoja cha utunzaji wa fedha IFM jambo ambalo liliwafanya kuwa karibu na kuamua kufanya kazi pamoja.

Ingawa kukutana kwake na Rommy ni tofauti na alivyokutana na Nicolass Nana kwani wao walikutana katika tamasha ambalo liliandaliwa na Aneth Kushaba na baada ya tamasha waliamua kukaa na kukubaliana kufanya kazi pamoja .

Kukutana kwao na mwanadada Loyce, aliletewa na mtu kutoka kundi la muungano wa wasanii wa chuo cha uhasibu(TIC) baada ya kuona The unique Band wana uhitaji wa msichana katika kundi lao.

“Siku ambayo tunamsikiliza Loyce akiimba alinivutia jambo lilifanya kumpatia nafasi ya kujiunga katika kundi hili,” alisema Alex.

Matarajio yao

Licha ya kukumbwa na changamoto nyingi katika shughuli za kimuziki kundi hili limejiwekea mikakati inayoweza kuwanufaisha na kuwafanya watu wote wafanikiwe kupitia vitu wanavyovipenda bila ya kundi kuvunjika.

Meneja Masoko kutoka The Unique band, ‘Nicolass Nana’ anasema ni ngumu kwa mtu kuendelea peke yake hivyo wanakaa katikakundi ili kuweza kusaidiana katika mambo mbalimbali ili kila mtu aweze kufanikisha kile anachokihitaji.

“Tunasaidiana kimawazo na mambo mbalimbali ili mwisho wa siku kila mmoja aweze kusimama na kitu chake lakini bendi ikiwa bado inaendelea” alisema Nicolass Nana na kuongeza kuwa

“Kukaa katika kundi kunafanya mambo kuwa mepesi kwa sababu kuna baadhi ya vitu mimi sivifahamu ila Alex anafahamu, mimi sijui kupiga gitaa ila Rommy anajua pia naweza kuwa sijui jinsi gani ya kukifanya kitu fulani lakini Loyce anafahamu hivyo tunajikuta tuna faida nyingi kuliko kuwa peke yangu,” alisema Nicolass Nana.

Mpaka sasa hawajaweza kutunga wimbo wao lakini wanaimba nyimbo za wasanii mbalimbali wa bongo flave na rnb wakati wakiwa katika mchakato wa kuandaa nyimbo zao.

Malengo yao ni kuwa bendi kubwa itakayotumbuiza katika majukwaa makubwa.

“Bado tunajijenga, unajua sasa hata watu kutuamini kutupa kazi inakuwa ngumu kwa sababu ndio tunaanza, lakini tumejipanga kulikamata soko la muziki,” alisema Loyce.

Changamoto

Kila kazi ina ugumu wake vivyo hivyo kundi hili limekuwa likipata vikwazo lakini haviwakatishi tamaa.

“Ugumu wa kazi hii ni wakati kama huu ukiwa ‘underground’ tunajitahidi kutafuta masoko zaidi ili angalau kwa  wiki tufanye kazi kwa siku tatu,” anasema Loyce.