Wanamuziki wa kike vaeni nguo zenye staha

Muktasari:

Kipindi kilichokuwa kinarushwa hewani ni cha muziki uwe taarabu au dansi. Baaada ya kuona hivyo unaamua ujiliwaze kwa kujiburudisha kwa dakika chache huku ukingojea kuangalia taarifa ya habari ili kuelewa kilichotokea hapa nchini na kwengineko duniani.

 Fikiria umekaa nyumbani kwako nyakati za jioni ukiangalia televisheni ukiwa na familia yako. Tena wanafamilia hao wamo mzazi wako au wa mke wako na shemeji yako. Baada ya sekunde chache tu kuifungua runinga watoto wako nao wanasogea karibu kuangalia.

Kipindi kilichokuwa kinarushwa hewani ni cha muziki uwe taarabu au dansi. Baaada ya kuona hivyo unaamua ujiliwaze kwa kujiburudisha kwa dakika chache huku ukingojea kuangalia taarifa ya habari ili kuelewa kilichotokea hapa nchini na kwengineko duniani.

Mara unaona kinaonyeshwa kikundi cha wasichana ambao wapo robo tatu uchi, wanacheza muziki na kukata viuno kama vile ni watu ambao hawana akili.

Kwa bahati mbaya, hiyo runninga yako haina kitufe (remote control) cha kuingoza ukiwa mbali kidogo na kwa hivyo inakubidi uondoke kwenye kiti chako haraka kwenda kuizima au kubadili kituo. Hali inakuwaje hapo?

Nimewahi kupata simulizi ya kuchekesha, lakini inayosikitisha juu ya mzee mmoja alikuwa anatoka kuoga akiwa amefunga taulo kiunoni. Alipotupa jicho ukumbuni akitaka kuingia chumbani kwake aliona wajukuu zake wa wakiangalia wanenguaji wakiwa nusu uchi.

Huyu mzee, masikini alishituka na kuchanganyikiwa. Badala ya kuzima alivua taulo yake na kufunika kioo cha runinga na watoto kujikuta wanangalia maumbile ya babu yao. Masikini huyu mzee ….alitaka kuwalinda wajukuu zake na uchafu uiokuwepo kwenye rununinga na kumbe amefanya mabaya zaidi.

Hii ndio aina ya hali ambayo Rais John Magufuli hivi karibuni ameizungumzia kwa masikitiko makubwa na kuzungumzia kuporomoka kwa maadili ya Watanzania kunakoongezeka kwa kasi na kuonekanekana kukolezwa na baadhi ya wasanii wetu.

Dk Magufuli, kama walivyo Watanzania wengi, alihoji kama hali kama hiyo inakwenda sambamba na malezi, makuuzi na utamaduni wa Watanzania?

Jawabu lake haina haja ya kulisaka wala kulitafuta. Mwenendo huu haukubaliki katika maadili yetu ambayo hayataki hata mama na baba kupigana busu la mahaba hadharani kama wafanyavyo wazungu.

Mila, desturi na taratibu zetu za maisha zinaweka wazi mambo gani mtu anaweza kuyafanya hadharani na yepi sio mazuri kuyatenda mbele za watu, hasa watoto wadogo au wazee wako ambao unatarajiwa kuwaonyesha heshima na unyenyekevu.

Kwa kweli alichokieleza Rais kwa sauti ya masikitiko ndio kilio kikubwa kinachosikika sana siku hizi miongoni mwa Watanzania wengi ambao mwishowe hubaki kujiuliza: Taifa hili linaelekewa wapi?

Ukweli ni kwamba hali ilivyo siku hizi ni ya kusikitisha na kuisha na kama vile tumekuwa na jamii isiojuwa ilipotoka, haina heshima na maadili.

Haya hatuyaoni mitaani na makazini na zaidi miongoni mwa kizazi kipya, bali pia katika baadhi ya maneneo yanayotumika kwa burdani ya muziki, uwe wa taarab au dansi.

Fikiria inakuwaje katika jamii ya watu wanaojiita wastaarabu, waungwana na wenye kujiheshimu na wenye maadili kuwa na nyimbo zenye matusi na maneno machafu yanayotamkwa wazi wazi.

Kwa mfano, inakuwaje hata uwe na beti katika nyimbo isemayo tunacheza mechi bila ya jezi au panakuwepo maonyesho ya msichana anakata viuno ambavyo hata paka anapokuwa anafanya hivyo, hujificha juu ya dari ya nyumba au kwenye kichochoro na sio mbele ya watu.

Hapa tujiulize nani unawezakumwita mnyama, paka anayefanya mambo hayo kwa siri au binaadamu anayekata viuono hadharani?

Wakati umefika kwa Wtanzania kuitafakari hali waliokuwa nayo na kuifanyia marekebisho ya haraka ili kuiusu jamii ya hivi sasa na vizazi vijavyo.

Ipo haja ya kuwa na sheria zinazoeleweka na utaratibu mzuri wa kulinda heshima na maadili yetu. Vituo vyetu vya runinga vinapaswa kuacha kushabikia mwendo huu kwa kuonyesha muziki ambao wanenguaji wake wapo nusu au robo tatu uchi.

Nani kasema muziki haunogi mpaka mcheza dansi awe yupo nusu uchi au anafanya vitendo kuashiria kama vile tupo katika zoezi la kujamiiana?

Kwa upande mwengine, taasisi zinazosimamia masuala haya zinapaswa kupiga marufuku nyinbo au mitindo ya michezo ambayo inakiuka maadili ili kulinda heshima katika jamii.

Katika jamii nyingi masuala kama haya huwa na maeneo maalumu na wale wanaoshabikia huenda huko kuyafuata, sio mambo haya kuwafuata watu hata majumbani mwao wakiwa na familia zao, wakiwamo watoto.

Ni vizuri kila nyimbo ikapitiwa na kuangaliwa kama maneno yanayotumika sio ya matusi au hayatowi tafsiri chafu ambayo inakirihisha na masikio ya muungwana hayapendi kuyasikia.

Utaratibu huu pia utumike katika matangazo ya biashara kwa sababu baadhi ya matangazo badala ya kutangaza biashara yanahubiri lugha mbaya ambayo maeneno yake yanaposikika katika jamii watu hushindwa kuangaliana usoni.

Hivi karibuni, jamii imesikika ikilalamikia tangazo moja la kampuni ya simu za mkoni na watu wengi wamelieleza tangazo hilo kama ni matusi ya wazi kwa sababu maneno yaliotumika si ya kistaarabu,

Wasanii wetu wanaapswa wajipime na kujirekebisha na kuelewa vizuri mila, tamaduni na maadili ya Watanzania na kuhakikisha kwamba burudani wanayotoa inafurahisha na sio kukirihisha.

Kwa upande mwengie, siku hizi kumezuka mtindo wa kuonekana wasichana wanaotumika kufanya matangazo ya biashara kuzunguka mitaani katika magari yenye kupiga muziki kwa kelele na kukata viuno.

Wakati mwengine magari haya hufanya maonyesho yao yenye sura chafu katika maeneo yaliojaa watu warika tafauti kama vile karibu na shule, maofisi. masoko na hata pembezoni mwa nyumba za ibada.

Wakati mwengine huo muziki na ngoma ambazo wachezaji wake wapo nusu uchi hufanyika nyakati waumini wakiwa katika ibada kuomba maghfira kwa Mola wao.

Tusikubali kuigeuza jamii yetu kama vile ni nyumba ya ukahaba au danguro, tujaribu kwa uwezo wetu wote kurejea katika ustaarabu, uungwana, mila na desturi tulizorithi kizazi baada ya kizazi kutoka kwa wazazi wetu waliotutangulia.

Jamii hutakiwa kujivunia mambo mazuri na sio watu kwenda uchi au mambo yanayoshabikia ufuska na ukahaba.

Tujirekebishe haraka kabla ya kuja kujuta na kujiuliza kwa nini tuliamua kuweka kando ustaarabu, malezi, mila na utamaduni mzuri tuliorithishwa na wazazi wetu waiotutangulia.

Ni wajibu wa kila mmoja, awe kiongozi, mwandishi wa habari au msanii wakati wote kuhakikisha anachukua hatua muwafaka nyumbani kwake, mitaani na popote pale alipo kuendeleza mila, utamaduni na maadili mazuri na yenye kuvutia na kutunza heshia ya Mtanzania katika jamii yetu.

Tuseme basi na kuamua yaliopita si ndwele tugange yajayo. Tutafanikiwa kama tutafanya maamuzi ya hekima na busara.

Mungu ibariki na ilinde Tanzania na watu wake.