Yanga: Akili yetu sasa ni ligi

Muktasari:

Yanga imeachwa kwa pointi 11 na Simba inayoongoza Ligi Kuu Bara kwa sasa

Hawassa, Ethiopia. Yanga imesema baada ya kutinga hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho sasa akili yao wanaielekeza katika mechi za ligi kuhakikisha wanafanya vizuri na kutetea ubingwa wao.

Hayo yamesemwa na meneja wa Yanga, Hafidh Saleh akisema wanaweka kando furaha yao ya kutinga hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho na sasa kilicho mbele yao ni mchezo wa ligi dhidi ya Mbeya City.

Saleh alisema wanarudi katika ligi wakiwa na morali kubwa baada ya mafanikio hayo ambapo wanataka kuongeza presha kwa vinara wa ligi Simba.

"Tunarudi nyumbani hizi furaha za kutinga hatua ya makundi tutaziacha pale Uwanja wa Ndege na akili yetu sasa ni mechi za ligi hasa mchezo ujao,"amesema Saleh

"Simba wanaongoza ligi lakini bado haijaisha tunarudi kucheza mechi zet na wao wakicheza zao bingwa tutamjua mwisho wa msimu, lakini siyo sasa."