Usafi hupunguza fangasi kusambaa sikioni, kupunguza madhara mwilini

Muktasari:

  • Leo tunaangalia maambukizi ya fangasi sikioni ambayo mara nyingi hutokea nje ya sikio. Hutokana na maambukizi ya fangasi. Vimelea vya fangasi vinavyosababisha maradhi haya kwa watu wengi huwa vinatoka kwenye jamii mbili ambazo ni aspergillus na candida.

Licha ya umuhimu wake, yasipotunzwa vizuri, masikio huweza kupata maambukizi ya yatokanayo na fangasi au bakteria. Mara nyingi maambukizi ya fangasi hufananishwa na yanayosababishwa na bakteria.

Leo tunaangalia maambukizi ya fangasi sikioni ambayo mara nyingi hutokea nje ya sikio. Hutokana na maambukizi ya fangasi. Vimelea vya fangasi vinavyosababisha maradhi haya kwa watu wengi huwa vinatoka kwenye jamii mbili ambazo ni aspergillus na candida.

Huweza pia kutoka kwenye jamii nyingine za fangasi kama vile actinomyces, phycomycetes na rhizopus. Jamii zote hizi hupatikana kwenye mazingira yaliyotuzunguka lakini kwa wengi huwa hawana madhara kwa sababu kinga ya kawaida ya mwili huwa na uwezo wa kukabiliana nao na kuwazuia wasilete tatizo lolote.

Fangasi hawa huweza kuleta madhara kwenye masikio pale inapotokea kinga ya mwili imeshindwa kuwazuia wasifanye hivyo. Mara nyingi maradhi haya hutibiwa kama yamesababishwa na vimelea aina ya bakteria kwa mgonjwa kupewa dawa aina ya antibiotiki ambazo hazina uwezo wa kukabiliana na vimelea aina ya fangasi. Matibabu sahihi hutolewa baada ya dawa za antibaiotiki kushindwa kutibu tatizo.

Walio hatarini

Ingaw akila mmoja anaweza kuugua mafangasi wa sikio, kuna walio kwenye hatari kubwa ya kupata maambukizi haya. Wanaooga au kuogelea kwenye maji yasiyo safi yaani maji machafu wanajiweka kwenye kundi hili. Yanaweza kuwa maji ya bwawa la kuogelea ambayo hayatibiwa au kubadilishwa siku nyingi au yaliyotuhama. Ikiwezekana, inashauriwa kuyaepuka.

Wengine ni wanaotumia dawa za kutibu maradhi mbalimbali kwa muda mrefu. Hii ni kwa sababu matumizi ya dawa kwa muda mrefu hushusha kinga za mwili hivyo kuufanya mwili usiweze kukabiliana na maradhi yatakayojitokeza.

Watoto wadogo wapo kwenye hatari zaidi ya kupata maradhi haya kutokana na kutokua na kinga imara pamoja na kujihusisha kwao na michezo ambayo inawaweka kwenye mazingira yenye vimelea vingi vya maradhi haya.

Watu wenye umri mkubwa au wenye maradhi ya muda mrefu kama vile kisukari ambayo hushusha kinga ya mwili nao wapo kwenye hatari ya kupata maambukizi ya fangasi wa sikio.

Dalili

Maumivu ya sikio hasa linapoguswa, muwasho na kuvimba ni miongoni mwa dalili za fangasi hawa. Baadhi ya wagonjwa hutoa usaha mweupe, mweusi au wenye rangi ya manjano sikioni.

Baadhi ya waathirika hushindwa kusikia vizuri kwenye sikio lenye tatizo, kama lililopata maambukizi ni moja, wengine hupata hisia kama kuna kitu kimekaa sikioni na wapo ambao sikio au masikio huziba.

Endapo mgonjwa atahisi moja ya dalili hizi inashauriwa aende hopitali kuonana na daktari ambaye atamfanyia vipimo maalum vya maabara.

Baada ya kujiridhisha kuwa ugonjwa unatokana na maambukizi ya fangasi daktari atatoa matibabu yanayostahili.

Matibabu

Kwanza kabisa ni vyema kusafisha sikio na kuondoa usaha au chochote kilichoko kwenye sikio. Hii husaidia kuondoa baadhi ya fangasi waliosababisha tatizo.

Utaratibu wa kusafisha sikio lililoathirika unatakiwa urudiwe mpaka pale atapopona. Usafishaji huu hufanywa kwa kutumia dawa ya hydrogen peroxide ambayo huondoa uchafu uliojishikiza kwenye kuta za mfereji wa sikio.

Kama maradhi yamesababisha ngoma ya sikio kuchanika basi ni vyema usafishaji huu ukafanywa na daktari bingwa wa masikio, koo na pua.

Zaidi ya kusafisha masikio yaliyoathirika, daktari atatoa dawa aina ya fangasi (antifungal agents) ambazo zina uwezo wa kukabiliana na fangasi. Kumbuka dawa za antibaiotiki (antibiotics) hazina uwezo wa kukabiliana na vimelea vya fangasi.

Dawa zinazotolewa huwa ni za matone ambayo mgonjwa ataweka kwenye masikio yake kwa kufuata maelekezo ya daktari. Haishauriwi kutoa dawa za kunywa kwa lengo la kutibu maradhi haya. Kama mgonjwa ni mtu mzima na kuna hatari ya maradhi kusambaa huwa inashauriwa kutibiwa kwa dawa za kunywa au zile zinazowekwa kwenye mishipa.

Hii ina lengo la kuzuia uwezekano wa vimelea vya fangasi kusambaa mpaka ndani ya sikio na mfupa wa fuvu na kusababisha madhara makubwazaidi.

Kwa walio mbali na hospitali na ambao wanashindwa kwenda hospitali kuna namna nyingine za kutibu maradhi haya. Wanaweza kuhakikisha wanakausha sikio muda wote ili kuwanyima fangasi nafasi ya kushamiri kwani hufanya hivyo maeneo yenye joto na majimaji.

Kama utaweza kuhakikisha sikio ni kavu muda wote utasaidia kuzuia fangasi wasiongezeke. Jambo la tahadhari ni kutoingiza chochote sikioni kwani unaweza kukausha eneo la nje tu la sikio.

Ukiingiza kijiti cha kuondolea nta ya sikio utasaidia kuvisukumia ndani zaidi vimelea vya maradhi na kuhatarisha afya ya ngoma ya sikio.

Unaweza kuweka siki vilevile. Vimelea vya fangasi hushindwa kushamiri na kuongezeka kwenye mazingira yenye tindikali. Siki (vinegar) ina tindikali hivyo ukiiweka kwenye sikio basi huondoa mazingira rafiki kwao.

Madhara

Matumizi ya dawa sahihi dhidi ya vimelea vya fangasi huwa yana matokeo chanya. Hii ina maana kuwa dawa za kukabiliana na vimelea vya fangasi huwa zinafanya kazi.

Sababu ya maradhi ya fangasi kusumbua kwa muda mrefu huwa ni kutokana na uwepo wa vimelea hivi kwenye mazingira yanayotuzunguka hivyo mara tu baada ya kumaliza dozi ya dawa, vimelea hivyo hupata upenyo wa kurudi kwenye eneo vilipoleta madhara na kuendelea kuleta madhara.

Ili kuepuka kurejea tena kwa maradhi ni lazima kwa mgonjwa kuhakikisha anahakikisha masikio hayawi na majimaji na kuyaweka kwenye hali ya usafi muda wote.

Endapo mgonjwa hatopata dawa sahihi kwa wakati vimelea vya fangasi vinaweza kusambaa na kuingia ndani ya sikio na kwenye mfupa wa fuvu na kuleta madhara makubwa.

Ni vyema kwa mgonjwa kwenda hospitali mara tu anapohisi dalili za maradhi ya sikio. Hatua hii itawezesha matibabu kutolewa kwa wakati na kuzuia uwezekano wa maradhi kusambaa na kuleta madhara makubwa zaidi.