Hoja fedha za maendeleo yaahirisha kikao baraza la madiwani

Muktasari:

  • Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Juma Porini alilazimika kuchukua uamuzi huo baada ya kuibuka malumbano kati ya madiwani, upande mmoja ukitaka suala hilo lijadiliwe na kuamuliwa na baraza katika kikao cha kawaida huku mwingine ukitaka baraza ligeuke kuwa kamati.

Hoja ya Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara kutotenga asilimia 60 ya fedha za makusanyo ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo imelazimisha kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kuahirishwa.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Juma Porini alilazimika kuchukua uamuzi huo baada ya kuibuka malumbano kati ya madiwani, upande mmoja ukitaka suala hilo lijadiliwe na kuamuliwa na baraza katika kikao cha kawaida huku mwingine ukitaka baraza ligeuke kuwa kamati.

Malumbano hayo yalifuatiwa na taarifa ya kamati ya madiwani wa Chadema inayoongoza halmashauri hiyo iliyowasilishwa na katibu wao, Francis Garatwa kuwa ofisi ya mkurugenzi haijawasilisha taarifa kwenye kamati ya fedha kuonyesha kiasi kilichotengwa kutekeleza miradi ya maendeleo.

“Baada ya taarifa hiyo kushindikana kuwasilishwa kwenye kikao cha kamati cha Desemba 29, 2017, Ofisi ya Mkurugenzi iliwasilisha taarifa inayoonyesha zimetengwa Sh382 milioni bila kuonyesha miradi iliyotekelezwa au inayokusudiwa kutekelezwa kwa fedha hizo,” amesema Garatwa.

Diwani huyo amesema katika uchunguzi wa awali, zaidi ya Sh320 milioni zilizostahili kuelekezwa kwenye miradi ya maendeleo haijulikani zilipo na kuomba baraza lijibadilishe na kuwa kamati ili kujadili suala hilo.

Hoja hiyo ilipingwa na watendaji wakiongozwa na mwanasheria wa halmashauri, Maganiko Msabi wakiungwa mkono na Mwakilishi wa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Samson William wakipendekeza suala hilo lijadiliwe katika baraza la wazi badala ya kamati.

Mbunge wa Serengeti, Marwa Ryoba aliunga hoja ya ofisi ya taarifa ya mipango na utekelezaji kuwasilishwa ili kuwapa madiwani fursa ya kujadili kwa ufasaha na kutoa mapendekezo kwenye bajeti ijayo kwa kuzingatia mafanikio na changamoto ya bajeti inayoishia Juni 30.

Baada ya malumbano ya zaidi ya saa nzima, mwenyekiti alilazimika kuahirisha kikao hicho kwa muda kutoa fursa kwa viongozi kujadiliana njia muafaka ya kukwamua mkwamo huo.

Januari 18, mbunge Ryoba aliwasilisha suala hilo mbele ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati wa ziara yake wilayani Serengeti ambapo kiongozi huyo aliuagiza uongozi wa halmashauri kutekeleza takwa la kutenga asilimia 40 hadi 60 ya pato la ndani kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa sababu ni suala la kisheria lisilohitaji mjadala.