Madaktari 159 tayari waomba kwenda Kenya -VIDEO

Muktasari:

 

  • Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema serikali ya Kenya na nchini Tanzania tayari zimekaa pamoja na kupanga mikakati mbalimbali kuhusu usalama na malipo ya madaktari watakaopatiwa ajira nchini humo.

Dar es Salaam. Wakati Chama cha Madaktari (MAT) kikikataa kutoa madaktari kwa ajili ya kwenda kuhudumu nchini Kenya, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema tayari imepokea maombi 159 kwa walio tayari.

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema serikali ya Kenya na nchini Tanzania tayari zimekaa pamoja na kupanga mikakati mbalimbali kuhusu usalama na malipo ya madaktari watakaopatiwa ajira nchini humo.

 Alisema licha ya upungufu wa madaktari nchini bado serikali ina uwezo wa kuajiri madaktari 500, lakini kwa kuwa kuna madaktari waliokidhi vigezo 2000 bado wapo mtaani na hawana ajira, hivyo maamuzi yaliyofanywa ni sahihi.

 " Marais hawa wawili wameshakubaliana na suala la usalama limeshahakikishiwa, inapozungumzwa kwamba MAT hawakushirikishwa sidhani kama ni sahihi kwa Rais John Magufuli kuanza kushirikisha taasisi katika hili haya ni maamuzi ya serikali hizi mbili na zimeridhia, ulinzi Upo wa kutosha na Rais Uhuru Kenyatta amelithibitisha hilo," alisema Ummy Mwalimu.