Marekani yataka malalamiko ya wagombea Kenya yashughulikiwe kwa mujibu wa katiba

Nairobi. Serikali ya Marekani imetahadharisha kuwa malalamiko ya wagombea kuhusu kasoro za uchaguzi yashughulikiwe kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi na si kwa kuhamasisha machafuko.

Hayo yamo kwenye taarifa iliyotolewa na msemaji wa Serikali kupitia ubalozi wao nchini hapa kwa kuwataka wadau wote wa uchaguzi kushughulikia kasoro zitakazo jitokeza kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi.

Taarifa hiyo pia ilivitaka vyama vya siasa na wafuasi wao kuwa watulivu wakimsubiri matokeo rasmi yatakapotangazwa na IEBC.

Marekani pia, imetaka IEBC imepewe nafasi ya kukamilisha kazi yake ya kukusanya matokeo na kuyatangaza kwa uwazi.

Taarifa hiyo iliitaka IEBC kuwa wazi katika kutangaza matokeo na kuchunguza madai yanayolalamikiwa kuhusiana na kasoro zilizojitokeza katika uchaguzi.

Pia, taarifa hiyo imewapongeza wananchi wa Kenya kwa kufanya uchaguzi kwa amani na kueleza kuwa Marekani imekuwa ikifuatilia kwa karibu uchaguzi huo ikiwamo kutuma waangalizi.