Magufuli: Ushuru ni ugonjwa

Rais John Magufuli

Muktasari:

Ametoa kauli hiyo leo Machi 10, 2018 wakati wa uzinduzi wa barabara ya kilometa 45 kutoka Uyovu hadi Bwanga wilayani Bukombe, mkoani Geita iliyojengwa kwa kiwango cha lami

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amesema ushuru ni ugonjwa ambao umeendelea kuwa kero kwa wafanyabiashara ndogondogo nchini.

 

"Ushuru ni ugonjwa , kila sehemu ushuru, ushuru , wabunge wenu wameshapitisha sheria. Mtu akiwa na chini ya tani moja ya mzigo asitozwe ushuru. Kwenye minada kulikuwa hata na ushuru wa kwato za ng'ombe, hivi unaweza kulizuia ling'ombe lisiwe na kwato?, “ amehoji Rais Magufuli.

 

Ametoa kauli hiyo leo Machi 10, 2018 wakati wa uzinduzi wa barabara ya kilometa 45 kutoka Uyovu hadi Bwanga wilayani Bukombe, mkoani Geita iliyojengwa kwa kiwango cha lami.

 

Barabara hiyo ilikamilika ujenzi wake Oktoba, 2017 na imejengwa kwa fedha za ndani kwa ajili ya asilimia 100.

 

Huku akizungumza mara kwa mara Kisukumu na kuwafanya wananchi waliohudhuria uzinduzi huo wa barabara kuangua kicheko, Magufuli pia alikemea kundi la watu aliodai kuwa hawapendezwi na kasi ya mafanikio katika sekta mbalimbali.

 

"Kuna watu hawapendi kuona amani hii tuliyonayo. Dhana halisi ya kutunza amani, amani ni kitu muhimu, hata mitume walihubiri amani, Yesu aliwaambia nawaachieni amani, kwa hiyo nawaambia amani tuliyonayo imejengwa na Mwalimu (Julius Nyerere), amekuja Mwinyi (Ali Hassan) na akaja KIkwete (Jakaya) pia ameitunza amani,” amesema.

 

"Tuwazuie dhahabu, tutengeneze reli kutoka Dar ,Dodoma, mpaka Lusumo na iwe ya umeme, nani anafurahi? Nani afurahi kuona barabara za lami zikijengwa?.”