Lembeli arejea CCM

Muktasari:

Maria Lembeli (80), mama mzazi wa mbunge huyo wa zamani amemtaka kutangaza kurejea CCM.


Kahama. Mbunge wa zamani wa Kahama, James  Lembele ametangaza kurejea CCM.

Ametangaza uamuzi huo leo Juni 13, 2018 muda mfupi baada ya kutangaza kuachana na siasa akidai ni kwa sababu ya kubanwa na utaratibu wa mashirika ya kimataifa anayofanyia kazi yasiyotaka mtu anayejihusisha na siasa.

Mbunge huyo wa zamani wa Kahama kwa miaka 10 amefikia uamuzi huku akilia baada ya mama yake mzazi, Maria Lembeli (80), kumshurutisha hadhari kurejea CCM.

Maria ameeleza kusononeshwa na uamuzi wa mwanaye kuhamia Chadema mwaka 2015.

Kauli hiyo ilipokewa kwa nderemo na vifijo na watu umati uliohudhuria shughuli hiyo

Awali, Lembeli alitangaza kuachana na siasa akitaja sababu kuu mbili; kwanza, mashirika na taasisi anazofanya nazo kazi zimemwambia achague moja kubaki kwenye siasa au kuendelea kushirikiana na taasisi hizo.

Akizungumza nyumbani kwake katika kKjiji cha Mseki, kata ya Bulungwa wilayani Ushetu, alisema sababu ya pili iliyomfanya aachane na siasa ni matatizo ambayo familia yake inayapitia baada ya yeye kujiunga na Chadema.