Ukusanyaji wa mapato wafikia Sh 21 trilioni 2017/18

Viongozi mbalimbali wakiwemo mabalozi na wakuu wa taasisi mbalimbali za kimataifa wakisoma vitabu vya hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/2019, ilipokuwa ikiwasilisha bungeni na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Mpango amesema Serikali ilikopa jumla ya Sh4.9 trilioni sawa na asilimia 80 

Dodoma. Waziri wa Fedha, Dk Philip Mpango amesema ukusanyaji wa mapato katika vyanzo vyote kwa mwaka 2017/18 yalifikia Sh21.89trilioni sawa na asilimia 69 kwa mwaka.

Ameyasema hayo leo Juni 14, wakati akisoma bajeti kuu  ya serikali kwa mwaka wa fedha, 2018/19.

Amesema kutofikiwa kwa malengo ya ukusanyaji kumetokana na ukwepaji wa kodi, ugumu wa kukusanya kodi kutoka kwa wafanyabiashara wasio rasmi na hawarunzi kumbukumbu, mazingira yasiyo rafiki ya kukusanya kodi, ugumu na gharama kubwa za kulipa kodi.

Ametaja sababu nyingine kuwa ni pamoja na udhaifu wa kutumia mashine za EFD, mpango mdogo na utegemezi wa sekta ya umma kwa sekta binafsi.

Kuhusu mikopo ya ndani, Dk Mpango amesema Serikali ilikopa jumla ya Sh4.9 trilioni sawa na asilimia 80 ya zilizotarajiwa kukopwa na Serikali ilikopa kutoka soko la nje Sh414 bilioni.

"Fedha hizi zimeelekezwa kwenye miradi ya mkakati," alisema Dk Mpango.

uhusu deni la Serikali, alisema limekuwa likiongezeka lakini bado ni himilivu.

"Uwiano kwa pato la Taifa ni asilimia 34 ukilinganisha na asilimia 56 ya ukomo," amesema.

Amesema Serikali imeandaa mkakati wa kulipa madeni na kuzuia ulimbikizaji wa madeni kama wakandarasi na wazabuni.