Airtel kuanzisha maabara ya kompyuta

Muktasari:

  • Mafunzo hayo yametolewa na walimu sita kutoka Kituo cha Elimu cha Galway cha nchini Ireland kwa lengo la kuwapatia uwezo, mbinu na maarifa ya teknolijia ya kompyuta ili kuwafundisha wanafunzi watakaojiunga na kutembelea maabara.

Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel kwa kushirikian na Atamizi Teknohama ya Dar es Salaam (DTBi) wametoa mafunzo kwa walimu wa shule za msingi na sekondari ikiwa ni katika matayarisho ya kufungua maabara ya kompyuta yanayotegemea kuzinduliwa mwezi huu.

Mafunzo hayo yametolewa na walimu sita kutoka Kituo cha Elimu cha Galway cha nchini Ireland kwa lengo la kuwapatia uwezo, mbinu na maarifa ya teknolijia ya kompyuta ili kuwafundisha wanafunzi watakaojiunga na kutembelea maabara.

Kwa kutumia ujuzi huo, walimu hao wataweza kutengeneza programu ndogo ndogo na baadaye kuvumbua programu kubwa zenye kuleta suluhisho kwa mahitaji mbalimbali ya biashara na jamii

Maabara ya Airtel Fursa itatatoa fursa kwa vijana wenye malengo ya kujifunza masomo ya tehama kuongeza ujuzi na kutoa mwanga kwa vijana kuwa wabunifu kwa kuzindua ‘application’ mbalimbali ambazo zitaweza kuwaingizia kipato.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkurugenzi Mkuu wa DTBi chini ya Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), George Mulamula alisema: “Kutokana na changamoto iliyopo sasa ya wanafunzi wengi kutumia kompyuta kwa mara ya kwanza wanapoanza masomo ya chuo kikuu kumefanya kuwe na ufinyu katika ubunifu na kutumia teknoloJia katika ujasiriamali. Tunaamini maabara ya Airtel Fursa yatatoa mwanya kwa vijana kujifunza masomo na kuvumbua mambo mengi wakiwa katika umri mdogo.”

“Mafunzo haya kwa walimu tunayotoa leo ni uthibitisho wa dhamira yetu katika kuhakikisha tunakuwa na walimu bora watakaowasaidia wanafunzi kujikita kwenye teknolojia na kuwa wabunifu,’’ aliongeza Mulamula.

Kwa upande wake Meneja Huduma Jamii wa Airtel, Hawa Bayumi alisema: “Tumejipanga kuwawezesha vijana kuzifikia ndoto zao kwa kuanzisha maabara hii yenye kompyuta za kujifunzia na kuwawezesha wanafunzi kujifunza mafunzo mbalimbali yatakayowawezesha kutanua wigo wao.”