Ajali ya barabarani yaua mwanafunzi Mbagala

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Gilles Muroto .

Muktasari:

  • Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Gilles Muroto amesema gari lililo wagonga watoto hao ni aina ya Suzuki Escudo na dereva aliyesababisha ajari hiyo tayari anashikiliwa na jeshi la Polisi.

Dar es salaam. Wanafunzi wawili wa Shule ya Msingi Kibonde wamegongwa na gari asubuhi na mmoja kufariki papo hapo wakati wakivuka barabara kuelekea shuleni hap leo asubuhi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Gilles Muroto amesema gari lililo wagonga watoto hao ni aina ya Suzuki Escudo na dereva aliyesababisha ajari hiyo tayari anashikiliwa na jeshi la Polisi.

“Asubuhi watoto wawili  Anwali Ally na Idrisa Sabo wakivuka barabara kuelekea shuleni waligongwa na gari eneo la Kibonde maji ambapo Anwali alipoteza maisha pale pale na kuwa taarifa za mwisho nilizonazo ni kwamba Idrisa Sobo amevunjika mguu wa kushoto na amelazwa katika hospitali ya Temeke,” amesema.

Hata hivyo, amesema kuwa baada ya ajari hiyo ilibidi kuweka askari mmoja wa usalama barabarani kwaajili ya kuwavusha watu kutokana na wananchi kukusanyika huku wakilalamika kuwa ajali hiyo ni matokeo ya kukosekana kwa matuta ya kupunguza mwendo.

Mkuu wa wilaya ya Temeke Felix Lyaniva amesema alifika kwa wafiwa na kuwapa pole huku akiahidi ujenzi wa matuta ndani ya wiki moja.

“Pale kuna alama ya kivuko cha watembea kwa miguu lakini hakionekani vizuri na ni eneo la mteremko nimeagiza kuwekwa kwa trafiki wa muda lakini vile vile ujenzi wa matuta uanze mara moja na kukamilika mapema,”amesema Lyaviva.

Shuhuda wa ajali hiyo Juma Rungu ambaye pia ni Mjumbe wa Serikali ya mtaa wa Kibonde maji amesema gari hilo lilikuwa katika mwendo kasi liliwagonga wanafunzi hao ambao walikua wakivuka kwakukimbia.

“Walikuwa ni wanafunzi watatu walivuka barabara kwa kukimbizana wakwanza alivopita alikutana na gari ikamgonga na kufariki pale pale, wapili naye ikamsukumia pembeni lakini alivopelekwa hosipitali baada ya muda naye alifariki lakini mwenzao hakudhurika kwa namana yoyote,”amesema Rungu.

Aidha Rungu amesema mara baada ya kutokea kwa ajali hiyo wananchi walikusanyika na kujaa barabarani wakishinikiza ujenzi wa matuta katika eneo hilo suala lililomlazimu Mkuu wa Wilaya ya Temeke kuingilia kati.

Hata hivyo Rungu alisema eneo hilo limekithiri kwa ajali kwani hakuna matuta ya kupunguza mwendo licha ya kwamba wananchi wanalalamika kila kukicha.