Askari mstaafu JWTZ ajinyonga kwa shuka hadi kufa

Muktasari:

Askari mstaafu wa JWTZ ametumia shuka kujinyonga  na mwili wake umekutwa kwenye chumba chake cha kulala usiku wa kuamkia leo.

Ngara. Askari  mstaafu wa Jeshi  la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Eliasi Kazoya  (68)  mkazi wa  kijiji cha Mukibogoye wilayani hapa amejinyonga kwa kutumia kipande cha shuka.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Mukibogoye wilayani Ngara Poncian Duguza  amesema askari huyo amejinyonga usiku wa kuamkia leo Septemba 14 na kwamba alijininginiza  juu ya paa  katika chumba chake cha kulala.
Duguza  pamoja na ndugu jamaa na marafiki za mwanajeshi huyo wamesema Kazoya aliugua kwa muda mrefu maradhi ya Kifua Kikuu.
“Nimepata taarifa za mwanajeshi mstaafu huyu kujinyonga baada ya wanafamilia kufika nyumbani kwangu kunijulisha majira ya saa 12 asubuhi na mimi  nikawafahamisha polisi,” amesema Duguza.

Akizungumzia tukio hilo, mke wa Marehemu Julitha Elias amesema pia mume wake aliwahi kusema kuwa atajiua.

“Kabla ya kujiua Septemba 13 alimtuma mwanaye wa darasa la saba kwenda kumnunulia wembe  ambao aliutumia kukata kipande cha shuka,” amesema na kuongeza:
“Niliishi naye  akiwa na maradhi haya ya kifua kikuu  na alipokuwa akienda Hospitali   kupewa dawa alipuuzia kumaliza dozi  na ameniacha  mjamzito  na nina watoto wengine saba,” amesema  Julieth.
Mkuu  wa Kituo cha Polisi Kabanga (OCS), Benard Masakia  ameshauri   wananchi   kutojichukulia  sheria mkononi bali wawashirikishe ndugu , jamaa na marafiki  kutafuta suluhisho.