Aua mkewe naye ajiua kwa kujinyonga

Muktasari:

  • Kutokana na tukio hilo, jamii imeaswa kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi na kuwaasa ndugu na viongozi wa dini kutatua migogoro ya kifamilia kabla haijawa mikubwa.

Songea. Siamini Fulgence (34) amemuua mkewe Asunta Michael (27), mkazi wa Kijiji cha Mtenje Vichakani wilayani Nyasa kisha naye akajiua kwa kujinyonga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Gemini Mushi amesema tukio hilo lilitokea jana saa sita mchana.

Kamanda Mushi amesema leo, Julai 25 kuwa mwanaume huyo alimuwekea mkewe nguo mdomoni na kumbana hadi akafariki dunia.

Amesema baada ya kumuua mkewe, Fulgence alijinyonga kwa kutumia kamba ya manila aliyoifunga kwenye mti hatua 10 kutoka eneo alilomuua mkewe.

Kamanda Mushi amesema chanzo cha mauaji hayo imebainika kuwa ni matatizo ya kifamilia.

Ameiasa jamii kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi na badala yake wayatumie madawati ya jinsia kutatua migogoro ya kifamilia.

Mushi amesema viongozi wa dini, jamii na ndugu wasaidie kutatua mgogoro kabla haujawa mkubwa ili kuzuia mauaji ama mtu kumdhuru mwingine au kujidhuru.