Daktari ajiua kwa kujinyonga na taulo

Muktasari:

Dk Banikira alikuwa amehamishiwa kikazi mkoani humo, miezi minne iliyopita.


Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kakonko, mkoani Kigoma ,  Mejo   Banikira (43) amekutwa amejinyonga chumbani kwake kwa kutumia taulo yake.

Hayo yamebainishwa leo Mei 29 na Mkuu wa Wilaya ya Kakonko, Kanali Hosea Ndagala wakati akizungumza na wanahabari.

Ndagala amesema   uchunguzi unaendelea ili kubaini chanzo cha daktari huyo kujiua.

“Mwili  wa Dk Banikira  umeondolewa nyumbani alikojinyongea  na kwenda kuhifadhiwa Hospitali ya Kibondo wakati jeshi la polisi likiendelea na uchunguzi,” amesema.

Amesema taarifa za kujinyonga zimepatikana asubuhi baada ya mke wake anayeishi kwingine, kupiga simu kwa muda mrefu bila kupokewa.

“Alipoona simu haipokewi, aliwapigia majirani ambao walikwenda na kukuta milango imefungwa, wakaripoti polisi na polisi ndiyo waliobaini mwili wake,” amesema Ndagala.

" Watu wasichukulie kujinyonga kuwa suluhisho la matatizo katika familia bali waeleze masahibu yao kwa marafiki na viongozi waweze kusaidiwa na kurejea maandiko ya misikitini au makanisani,"amesema Ndagala.

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Kakonko, Joseph Tutuba amesema marehemu alikuwa akiishi peke yake katika nyumba za kupanga mjini Kakonko na alikuwa amewasili kituoni hapo miezi minane iliyopita akitokea wilayani Simanjiro.