Dk Slaa: Tanzania ni dhaifu kupambana na mihadarati

Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbroad Slaa 

Muktasari:

Amesema hakuna mwamko wa dhati wa kuwahukumu kisheria wanaosafirisha dawa za kulevya

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbroad Slaa amesema Serikali imekuwa dhaifu katika kupambana na biashara ya dawa za kulevya hali inayosababisha vijana kuendelea kujiingiza katika uhalifu huo.

Dk Slaa alisema hayo hivi karibuni alipomkaribisha nyumbani kwake, Padri John Wootherspon kutoka Hong Kong aliyekuja kuhimiza kampeni ya kuwazuia vijana kuacha kusafirisha dawa hizo katika majimbo ya China ya Guangzhou, Macau na Hong Kong.

Padri Wotherspon ambaye anawatembelea wafungwa katika magereza ya Hong Kong, Macau na Guangzhou alisema kwa sasa kuna wafungwa wa Kitanzania zaidi ya 130 wanaotumikia vifungo kutokana na kusafirisha dawa za kulevya.

“Nitahakikisha kuwa unafanyika utaratibu wa kuwaondoa Watanzania waliofungwa Hong Kong warudishwe na kuhukumiwa nyumbani. Hilo jambo nitalipa kipaumbele kwa nafasi yangu,” alisema Dk Slaa.

Kuhusu wajibu wa Serikali katika kupambana na biashara hiyo, Dk Slaa alisema bado kuna udhaifu mkubwa kwani hakuna mwamko wa dhati wa kuwahukumu kisheria wanaosafirisha dawa za kulevya.

“Ikiwa Umoja wa Mataifa umekubali na kuidhinisha kuwa wafungwa wanaokamatwa nje ya nchi wahukumiwe katika nchi zao, iweje leo hapa nchini tusifanye mchakato wa kuwarudisha nyumbani hao ndugu zetu?” alisema Dk Slaa.

Katika mkutano huo, Dk Slaa aliandika ujumbe mfupi wa maneno kwa wafungwa hao akiwatakia maisha marefu na kuwaombea kumaliza salama vifungo vyao.

“Wadogo zangu, ndugu, dada na kaka zangu, kupitia Father John, nawaombea kwa Mungu awape ustahimilivu na atawaokoa kwa uwezo wake. Tupo nanyi,” ulisema ujumbe wa Dk Slaa.

Dk Slaa pia alisoma barua za wafungwa hao zilizoandikwa kwa mkono.

Padri Wootherspon alisema kukutana na Dk Slaa ni sawa na kukutana na kiongozi kama; Nelson Mandela au Mwalimu Julius Nyerere.

“Kwa dakika 90 nilizokaa pale na Dk Slaa nilijisikia kama nipo nyumbani kwa Mandela au Nyerere. Ninachoomba ni kuwa kwa nafasi yake asaidie vijana kuacha kusafirisha dawa za kulevya,” alisema.

Padri Wootherspon ambaye ameondoka jana kuelekea Hong Kong alisema ataendelea kufanya kila awezalo ili Tanzania isiwe kichochoro cha kusafirisha dawa za kulevya.