Kamishna wa Tume ya Uchaguzi Kenya ajiuzulu akiwa Marekani

Aliyekuwa Kamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) nchini Kenya, Dk Roselyn Akombe aliyetangaza kujiuzulu nafasi hiyo leo.

Muktasari:

Amejiuzulu zikiwa zimebakia wiki mbili kufanyika uchaguzi wa marudio

Nairobi, Kenya. Kamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) nchini Kenya, Dk Roselyn Akombe ametangaza kujiuzulu nafasi yake katika tume hiyo.

Dk Akombe ametuma taarifa ya kujiuzulu akiwa mjini New York nchini Marekani  anakoishi ambapo alikuwa akiufanyia kazi Umoja wa Mataifa kabla ya kujiunga na tume ya IEBC.

Katika taarifa yake, Akombe amesema kwamba  uchaguzi wa marudio wa uraisi uliopangwa kufanyika Oktoba 26 mwaka huu haujafikia vigezo vya kuwa uchaguzi huru na wa haki.

Akombe anajiondoa kwenye tume hiyo ya IEBC ikiwa imebaki wiki moja uchaguzi wa urais kurudiwa kutokana na matokeo ya awali kufutwa na mahakama kuu na kuamuru uchaguzi mpya ufanyike.

Agosti Akombe alizuiliwa kwenye uwanja wa ndege wa JKIA akielekea nchini Marekani.

Dk Roselyn Akombe Kwamboka alizaliwa 1976 katika kaunti ya Nyamira , na kusomea katika chuo kikuu cha Nairobi kabla ya kuelekea nchini Marekani kwa masomo zaidi.

Ana shahada ya uzamifu katika masuala ya sayansi na kimataifa mbali na shahada nyengine kama hiyo katika somo hilo kutoka chuo kikuu cha Rutgers .

Hadi uteuzi wake katika tume hiyo alifanya kazi kama katibu katika Umoja wa Mataifa mjini New York, wadhfa ambao anasema ulimwezesha kuwa na uzoefu katika maswala

Uwezo wake mkuu amesema mbele ya kamati ya bunge nchini Kenya, ni kutatua migogoro na kwamba ameishi ng'ambo kwa takriban miaka 15, hatua iliomwezesha kuelewa zaidi mahitaji ya watu wanaoishi ughaibuni wakati wa uchaguzi.