Kigwangalla auwasha moto Loliondo

Muktasari:

  • Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Ololosokwani, Dk Kigwangalla alisema mgogoro wa Loliondo uliodumu kwa zaidi ya miaka 26 sasa utapatiwa suluhu na Serikali. “Naomba wananchi muwe watulivu Serikali yenu inafanyia kazi matatizo ya Loliondo na kuhusu kampuni ya OBC kama ambavyo nilitaka leseni ya umiliki wa kitalu hiki ikimalizika mwezi Januari hatutawapa nyingine,” alisema.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamis Kigwangalla amesema siku za kampuni ya Ortello Business Cooperation (OBC) inayomilikiwa na Falme za Kiarabu kuendelea kuwapo katika Pori Tengefu la Loliondo wilayani Ngorongoro zinahesabika.

Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Ololosokwani, Dk Kigwangalla alisema mgogoro wa Loliondo uliodumu kwa zaidi ya miaka 26 sasa utapatiwa suluhu na Serikali. “Naomba wananchi muwe watulivu Serikali yenu inafanyia kazi matatizo ya Loliondo na kuhusu kampuni ya OBC kama ambavyo nilitaka leseni ya umiliki wa kitalu hiki ikimalizika mwezi Januari hatutawapa nyingine,” alisema.

Alisema kuna sababu nyingi za kutotoa leseni kwa kampuni hiyo ikiwamo kukiukwa kwa sheria ya vitalu ambayo hairuhusu kutolewa leseni katika eneo lenye mgogoro na pia ina eneo kubwa la kilomita za mraba 4,500 ambalo hawalitumii lote kutokana na kuwapo kwa makazi ya watu.

Akizungumza katika kikao hicho, mmoja wa wananchi wa Kijiji cha Ololosokwani ambacho kinapakana na kitalu cha OBC, Koya Timan alisema kampuni hiyo ambayo inapakana na Hifadhi ya Serengeti imekuwa ikiwazuia wafugaji kupata malisho na maji.