Kikosi kazi chaundwa kuzuia 'viroba' toka nje

Muktasari:

Kikosi kazi hicho, mbali na kufuatilia pia kitakuwa na jukumu la kufanya ukaguzi  na kitajumuisha  Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Fedha, Wizara ya Viwanda na Biashara,  Shirika la Viwango Tanzania (TBS) , Uhamiaji na  Polisi.

Dar es Salaam. Serikali imeunda kikosi kazi cha Taifa cha  kufuatilia pombe kali zinazofungashwa kwenye pakiti za plastiki 'viroba' zinazoingia mipakani kutoka nchi za nje.

Kikosi kazi hicho, mbali na kufuatilia pia kitakuwa na jukumu la kufanya ukaguzi  na kitajumuisha  Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Fedha, Wizara ya Viwanda na Biashara,  Shirika la Viwango Tanzania (TBS) , Uhamiaji na  Polisi.

Akizungumza na wanahabari (leo Jumatatu mchana), Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira, January Makamba amesema lengo la kuunda kikosi kazi hicho ni kudhibiti 'viroba' vinavyoingizwa nchini .

Amesema Serikali imeshatangazwa kupiga marufuku 'viroba' ifikapo Machi Mosi, mwaka huu hivyo mkakati huo lazima uende sambamba na kuzuia viroba vinavyotoka nje ya nchi.

"Doria za  ukaguzi wa utekelezaji  wa hatua hizi, utaanza wakati wowote  kuanzia sasa na hatua kali zitachukuliwa kwa wale wataobainika kukiuka,"amesema Makamba.