Kada Chadema ashinda udiwani akiwa gerezani

Muktasari:

Diwani huyo, Ameri Nkulu (56) alihukumiwa kwenda jela kwa miezi sita, siku mbili kabla ya wananchi kupiga kura kwenye Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25.

Sumbawanga. Kada mwingine wa Chadema ameukwaa uongozi kwa staili ya aina yake baada ya wananchi kumchagua kuwa diwani wa Kata ya Lusaka akiwa gerezani ambako anatumikia kifungo cha miezi sita kwa kosa la kupigana hadharani.

Huyo ni mwanachama wa tatu wa Chadema kuukwaa uongozi kwa staili ya aina yake. Wengine wawili waliteuliwa kuwa wabunge wa viti maalumu wakiwa wanaendelea na ajira zao CCM.

Diwani huyo, Ameri Nkulu (56) alihukumiwa kwenda jela kwa miezi sita, siku mbili kabla ya wananchi kupiga kura kwenye Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25.

Nkulu alipatikana hatia ya shtaka la kupigana na kiongozi wa CCM kwenye kata hiyo, Kristian Kafwimbi.

Lakini uamuzi huo wa Mahakama haukuwazuia wananchi wa Lusaka kumpa kura Nkulu.

Pamoja na sheria kutomzuia mtu anayepata kifungo cha chini ya mwaka mmoja kushika madaraka ya kuchaguliwa, Nkulu hatahudhuria vikao vya baraza la madiwani na kufanya shughuli nyingine za kuhudumia wananchi kwa kuwa anaendelea kutumikia adhabu hiyo.

Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Sumbawanga, Rozari Mugissa ndiye aliyetoa hukumu kwa Nkulu na mwenzake  kwa kutumia kifungu cha 87 cha Sheria ya Adhabu Sura ya 16 baada ya kuwakuta na hatia ya kupigana hadharani.

Katika kesi hiyo namba 33/2015, Nkulu alikuwa akitetewa na mwanasheria, Bartazari Chambi ambaye aliomba mteja wake atumikie adhabu nyingine badala ya kifungo, lakini hakimu hakukubaliana na ombi hilo.

Akizungumzia hukumu hiyo, mwanasheria wa kijitegemea, Mathias Bododi wa kampuni ya S. Mawalla Law Consulants, alisema kwa kosa la aina hiyo, sheria inaelekeza hukumu ya kulipa faini ya Sh500 au kifungo cha chini ya mwaka mmoja.

Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Emmanuel Kawishe alisema diwani huyo ataendelea na makujumu yake baada ya kumaliza adhabu kwa kuwa kifungo chake ni cha miezi sita ambacho ni chini ya kiwango kilichowekwa kisheria kwa mtu kupoteza sifa ya kuchaguliwa.

Alisema kama angefungwa zaidi ya kipindi hicho, angekosa sifa ya kuwa diwani. Alisema akimaliza kifungo ataapishwa na kuendelea kuwatumikia wananchi.

Hoja hiyo pia iliungwa mkono na wakili wa kampuni ya MM Law Chamber, Mohamed Menyanga aliyesema kifungo hicho hakimwondolei haki ya kuwawakilisha wananchi.