VIDEO: Lipumba: Serikali itangaze nchi kurejea mfumo wa chama kimoja

Muktasari:

 

  • Amesema hakuna maana kujiita nchi ya demokrasia wakati nguvu zinatumika kukifanya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuendelea kuongoza

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba ameitaka Serikali kutamka wazi kuwa Tanzania ni nchi ya chama kimoja ili kuwaondolea wapinzani usumbufu wa kushiriki uchaguzi.

Amesema hakuna maana kujiita nchi ya demokrasia wakati nguvu zinatumika kuifanya CCM kuendelea kuongoza.

“Kama vipi tuwe kama China tu lijulikane moja, nchi yetu ni ya chama kimoja cha siasa na tujifunze kutoka kwao (China) wanaendeshaje nchi kuliko haya yanayofanyika," amesema.

Kauli hiyo ya Lipumba imekuja kufuatia kuwapo kwa wanachama wa CUF waliotaka kugombea udiwani lakini wakumbana na hujuma ili wasishiriki.

Akizungumza leo Jumamosi Septemba 22, 2018 jijini Dar es Salaam,  Lipumba amesema wagombea hao kutoka Kibiti na Mkuranga walifanyiwa hujuma ikiwamo kunyimwa na kuporwa fomu na wengine kutekwa.

"Nataka niwapeleke wagombea hawa wakaelezee kule tume (Tume ya Taifa ya Uchaguzi-Nec) majanga yaliyowakuta isiwe watu wanajigamba wamepita bila kupingwa," amesema.

Lipumba ameyasema hayo wakati wa uzinduzi wa mkutano wa baraza kuu la chama hicho unaolenga kujadili mambo kadhaa.

"Hali si nzuri tusijidanganye, hii ni nchi yetu sote hakuna mtu kwenye nchi hii mwenye haki miliki lazima tujenge misingi ya demokrasia," amesema Lipumba na kuongeza:

“Chama chetu kinaamini kwenye demokrasia kila mtu awe huru ili mradi havunji sheria.”