Lipumba aiweka Ukawa njia panda

Profesa Ibrahim Lipumba

Muktasari:

Profesa Ibrahim Lipumba, aliyeiandikia CUF barua ya kujiuzulu uenyekiti wakati wa kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka jana kabla ya kutengua barua hiyo katikati ya mwaka huu, anataka kurejea kwenye kiti hicho.

Dar es Salaam. Mgogoro unaoendelea ndani ya Chama cha Wananchi (CUF) unauweka njia panda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), unaoundwa na chama hicho pamoja na Chadema, NCCR-Mageuzi na NLD.

Profesa Ibrahim Lipumba, aliyeiandikia CUF barua ya kujiuzulu uenyekiti wakati wa kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka jana kabla ya kutengua barua hiyo katikati ya mwaka huu, anataka kurejea kwenye kiti hicho.

Amesema anakusudia kufanya mabadiliko huku akiungwa mkono na kundi la wanachama wa jijini Dar es Salaam, waliovunja makomea ya geti la makao makuu ya chama hicho ili aingie ofisini baada ya Msajili wa Vyama vya Siasa kueleza maoni yake kuwa Profesa Lipumba bado ni mwenyekiti halali wa CUF.

Wakati CUF ikiendelea kuvutana na Profesa Lipumba, Makamu Mwenyekiti wa Chadema Bara, Profesa Abdallah Safari amesema mgogoro huo unaweza kuchangia kupunguza ushawishi wa Ukawa kwa kuwa ulianzishwa kutokana na utashi wa wananchi wakati wa mchakato wa kuandika Katiba mpya.