Lukuvi akesha ofisini akitatua migogoro ya ardhi

Muktasari:

  • Waziri Lukuvi amelazimika kuwaita watu wenye matatizo ya ardhi kutokana na kuongezeka kwa malalamiko kuhusiana na masuala ya ardhi

Dar es Salaam. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi leo  amelazimika kukesha ofisini kwake akiwahudumia wakazi wa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani waliowasilisha matatizo mbalimbali kuhusiana na ardhi.

Waziri Lukuvi aliingia ofisini majira ya saa mbili asubuhi siku ya Ijumaa lakini akajikuta akilazimika kufanya kazi hadi saa tisa usiku wa kuamkia leo Jumamosi.

Wananchi 189 wenye matatizo na kero za ardhi aliitikia wito alioutoa waziri Lukuvi mwezi Juni, akiwataka watu wote katika mikoa ya Dar es salaam na Pwani, wenye matatizo ya ardhi, kujiorodhesha ofisini kwake pamoja na anwani zao na angepanga siku ya kusghulikia matatizo hayo yeye mwenyewe binafsi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara, sehemu kubwa ya wakazi hao walilala nje ya ofisi za wizara hiyo jijini Dar es Salaam wakisubiri kuonana na waziri Lukuvi.

Wananachi wengi wenye matatizo na kero za ardhi waliokesha na Lukuvi walitokea Bagamoyo, Kibaha, Mkuranga, Kibiti na Dar es salaam.

Wananchi hao wamesifu hatua hiyo ya Waziri Lukuvi kukutana nao ana kwa ana na kuzitatua kero zao za ardhi kwa kuwa haijawahi kutokea.

Francis Kamara, mkazi wa Ilala jijini Dar es salaam, amemuomba Waziri Lukuvi awawajibishe watumishi ambao wanakwamisha jitihada zake hadi kusababisha yeye kukutana na wananchi moja kwa moja.