Lukuvi awaonya maofisa ardhi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi akiwaonya maafisa ardhi na maafisa mipango miji wasio waadilifu na kusababisha kero za migogoro ya ardhi nchini wakati wa uzinduzi Mpangomji wa mji wa Iringa.

Iringa. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi amewaonya maafisa ardhi na maafisa mipango miji wasio waadilifu na kusema siku zao za kuwarubuni wananchi zinahesabika.

Amesema kwa kiasi kikubwa, ufisadi unaofanywa na maofisa ardhi ndio chanzo kikubwa cha migogoro ya ardhi nchini.

Ameyasema hayo wakati akizunguza Mpangomji wa manispaa ya Iringa katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa shule ya sekondari Lugalo.

Amesema mchezo huo wa ufisadi ambao umekuwa ukitumiwa  miaka  yote na maofisa ardhi nchini ameubaini na kuwataka wakurugenzi wa Halmashauri nchini kutokubaliana na ramani za maeneo mapya zinazoletwa na wataalam hao bila ya wao kufika maeneo husika na kuoneshwa maeneo hayo ili kujiridhisha.

Waziri Lukuvi amefichua kuwa ufisadi unaofanywa na maafisa ardhi nchini kwa kupima viwanja  hewa kwa  ajili ya maslahi yao na kusema kuwa mbinu ambayo  wamekuwa  wakiitumia  kuiibia  serikali amekwisha  ibaini na  hatakubali  kuona mbinu  hiyo inapewa nafasi katika serikali  hii ya awamu ya  tano chini ya  Rais John Pombe Magufuli.

Lukuvi  amesema kuwa wathamini nao pia wamekuwa wakiwapunja wananchi wasio na uelewa kwa  kuwafanyia tathimini kubwa zaidi ya uhalisia wake.

“Wakati nilipokuwa Mkuu wa  Mkoa wa Dar es salaam nilibaini ujanja wa wathamini baada ya  eneo ambalo nyumba  zake zina thamani kati ya shilingi milioni 20 hadi 50  kwa maana  nyumba hizo ni za udongo  ila maofisa  hao  walimtafuta  mtu  na kutafuta nyumba  nzuri zaidi na kumshikisha  kibao  kisha kumpiga  picha na  kuandika kuwa  nyumba  hiyo inathamani ya  zaidi ya  milioni 200,” amesema.