Madereva bodaboda 74 wakamatwa

Muktasari:

Mbali na madereva hao, jeshi hilo linazishikilia pikipiki 67 sanjari na abiria sita waliovunja sheria wakiwa katika vyombo hivyo vya moto.

Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke, linawashikilia madereva wa pikipiki 74 maarufu ‘bodaboda’  kwa tuhuma mbalimbali ikiwamo kukikuka sheria za usalama barabarani.

Mbali na madereva hao, jeshi hilo linazishikilia pikipiki 67 sanjari na abiria sita waliovunja sheria wakiwa katika vyombo hivyo vya moto.

Kamanda wa Polisi wa Temeke, Gilles Muroto ameliambia  gazeti hili leo kuwa madereva , abiria na pikipiki wamekamatwa katika msako wa kuwatafuta madereva wanaovunja sheria za barabarani.

Amesema watu hao na vyombo hivyo, wadakwa katika maeneo ya Charambe, Mbande na Chamazi na miongoni mwa makosa mengine ni kutokuwa na leseni, kofia ngumu ‘helmet’ na kubeba mishikaki.